Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii
imelitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuhakikisha linatilia mkazo
ukusanyaji madeni ya wapangaji katika nyumba zake.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Timetheo Mnzava amesema, pamoja na
shirika hilo kujitahidi katika ukusanyaji malimbikizo ya kodi za wapangaji wake
lakini bado linatakiwa kuongeza kasi ya ukusanyaji madeni kutoka kwa wadaiwa.
Akizungumza wakati wa Kikao cha kupokea taarifa ya utendaji
kazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jijini Dodoma tarehe 25 Oktoba 2023,
Mhe. Mnzava amelitaka pia shirika hilo kuweka msisitizo zaidi katika kuzuia
kuzalisha madeni badala ya kusubiri mpaka wapangaji kuwa na malimbikizo makubwa
ya madeni.
Aidha, Wajumbe wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi
Malisili na Utalii wametaka kuwepo mikakati madhubuti itakayowaogopesha
wapangaji ili waweze kulipa kodi zao kwa wakati.
Vile vile, Kamati hiyo imeonesha kuridhishwa na utendaji
kazi wa shirika hilo katika kutekeleza miradi yake ambapo wamelitaka Shirika
kuangalia namna ya kujenga nyumba za gharama nafuu kwa kutumia teknolojia
rahisi.
‘’Niipongeze NHC pamoja na Wizara ya Ardhi maana kazi za
shirika zinaonekana hata kwa macho ila nisisitize muweke jitihada pia katika
ukarabati wa nyumba zenu ili wapangaji wakae vizuri,’’ alisema mjumbe wa kamati
Cecilia Paresso.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline
Mabula akizungumza mbele ya Kamati hiyo amesema, kwa sasa upo uhitaji mkubwa wa
nyumba na serikali iko katika marekebisho ya sera ili kuwezesha ushiriki wa
taasisi na sekta binafsi katika uzalishaji nyumba.
‘’Kama serikali tutahakikisha kasi ya ujenzi wa nyumba
inaongezeka maana takwimu za sensa ya watu na makazi zimeonesha uhitaji mkubwa
wa nyumba na uzalishaji ukiwa mdogo hivyo msisitizo ni kuzalisha nyumba za
gharama nafuu kwa kutumia teknolojia rahisi,’’ alisema Dkt. Mabula.
Na. Munir Shemweta- WANMM
0 Maoni