Wahandisi sekta ya usafirishaji wapatiwa mafunzo ya usimamizi wa miradi

 

Wahandisi kutoka Wizara na Taasisi zinazojihusisha  na usimamizi wa miradi ya usafirishji hususani ile ya miundombinu wapo Mkoani Arusha kwa ajili ya kupatiwa mafunzo  ya kuimarisha usimamizi wa miradi ili kupunguza gharama  na  ucheleweshaji wa miradi nchini.

Mafunzo hayo ya siku tano yameandaliwa na  Chama  cha Barabara Tanzania (TARA) ambapo wataalamu wabobezi kutoka Tanzania na Zambia  watawasilisha mada mbalimbali katika kuwajenga uelewa Wahandisi hao.

Akiongea wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mgeni rasmi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri kutoka Wakala ya Barabara za VIjijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Florian Kabaka amesema kuwa yapo mapungufu  makubwa kwa wataalam hususani wakati wa mikataba  inayopelekea hasara kwa serikali hivyo mafunzo hayo yatawasadia katika maeneo yao.

“Kumekuwa na matatizo mengi katika mikataba yetu, shida nyingi kwenye hiyo mikataba ikiwepo mikataba kubadilika ama kuzidi kiwango tofauti na bajeti zilizowekwa, madai yasiyokuwepo kwenye mikataba ya awali au kugundulika matatizo mengine yanayotokana na viwango vya kazi kubadilika kwasababu awali havikuwa vimejadiliwa vizuri na hivyo kupelekea kuipa hasara serikali," amefafanua.

Amesema kutokana na hali hiyo sekta ya usafirishaji kwa kushirikiana na TARA wameona ni vyema kufanya mafunzo hayo ili watendaji waweze kutekeleza mikataba kwa usahihi na ubora kuanzia pale miradi inapobuniwa hadi utekelezaji wake kukamilika.

Hata hivyo Mhandisi Kabaka ameshauri ni vyema wasimamizi wa miradi wanaochukuliwa hususan wale ambao hawana uzoefu ni vyema wakawa chini ya usimamizi wa wabobezi ili kuondokana na uwezekano wa kuiletea hasara serikali.

Naye, Mhandisi Pharles Ngeleja kutoka TARURA amesema kwamba upo umuhimu wa sekta ya usafirishaji  kukuwa kwa haraka hasa vijijini hivyo wao kama TARURA wameweza kufungua maeneo mengi hususan ya vijiji kwa kujenga miundombinu ya barabara ikiwemo madaraja kwa kutumia teknolojia ya mawe.

Amesema tangu kuanzishwa kwa TARURA  mwaka 2017  wamefanikiwa kujenga madaraja ya mawe takriban 453 na hivyo kuweza kuokoa fedha nyingi na vilevile wananchi wameweza kunufaika kiuchumi na kijamii.

“Katika maeneo mengi hivi sasa yamefunguka na hivyo wananchi wanaweza kufikia huduma za kijamii na kuweza kusafirisha mazao yao kwa urahisi na hivyo kuinuka kiuchumi,” amesema.

Mafunzo hayo ya siku tano yamehudhuriwa na wahandisi kutoka OR-TAMISEMI, Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Ujenzi, Road Fund, TARURA pamoja na TANROADS.





Chapisha Maoni

0 Maoni