DC Matinyi amuagiza Mkandarasi kukabidhi soko la Mbagala Zakhem Agosti 15

 

Mkuu wa Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam Bw. Mobhare Matinyi amemtaka Mkandarasi anayejenga Soko la kisasa la Mbagala Zakhem kuhakikisha anakamilisha na kukabidhi kabla ya Agosti 15 mwaka huu.

Bw. Matinyi ametoa maagizo hayo akizungumza mara baada ya kutembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa soko hilo la kisasa ambalo ujenzi wake umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.843.

"Namwagiza Mkandarasi kuhakikisha kuwa hadi kufikia Agosti 15 mwaka huu ujenzi wa soko hili uwe umekamilika na liwe limekabidhiwa," Alisema Bw. Matinyi.

Bw. Matinyi ameitaka Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kuhakikisha hadi kufikia Agosti 31 mwaka huu maombi ya wafanyabiashara walioomba vizimba na fremu za kufanyia biashara zao yawe yameshapitiwa tayari kwa ajili ya kuwagawia.

Alisema soko hilo ni la kisasa ambalo litachukua wafanyabiashara wengi tofauti na la awali ambalo lilikuwa limejengwa kwa mabati hali ambayo ilikuwa ni hatarishi kwa wafanyabiashara. Kwamba kwa sasa soko hilo litachukua zaidi ya wafanyabiashara 300 kwani lina vuizimba zaidi ya 136 na fremu 150, na amempongeza na kumshukuru mkandarasi kwa kuongeza sehemu ya mama lishe ambayo itakuwa na mama lishe 20.

"Kukamilika kwa Soko hili la kisasa pamoja na kuwa na ubora, litakuwa na uwezo wa kuwahudunia wafanyabiashara wengi zaidi na hadi sasa walioomba ni wafanyabiashara zaidi ya 3000," Alisema Bw. Matinyi.

Aidha, Bw. Matinyi pia ametumia ziara hiyo kuwahakikishia wafanyabiashara wote ambao awali walikuwa wakifanya shughuli zao katika soko hilo watarejeshwa wote na kisha ndio waaangalie maombi ya watu wengine, lakini pia watakaokosa wataendelea kuwaboreshewa maeneo mengine, lengo ni kuhakikisha kila mfanyabiashara anakuwa katika mazingira mazuri.

Hata hivyo amewataka wafanyabiashara watakaobahatika kufanya biashara zao katika soko hilo kuhakikisha wanatunza miundombinu yake, mazingira na kulipa kudi ya Serikali kwa uaminifu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Bw. Elihuruma Mabelya amesema soko hilo la kisasa limejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 2.843 na hadi sasa ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.

Amesema Halmashauri imejipanga kuhakikisha miundombinu ya soko hilo inatunzwa ili kuwanufaisha wafanyabiashara kwa kupata kipato pamoja na halmashauri kupata mapato pia.

Amewahakikishiwa wafanyabiashara kwamba ugawaji wa maeneo utafanyika kwa haki na asitokee mtu yeyote wa kuwarubuni kwa kuwataka watoe fedha ili wapatiwe maeneo.

Naye Mstahiki Meya wa Halmashuri ya Manispaa ya Temeke ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kibonde Maji ambapo ndipo soko hilo lililopo amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa soko la kisasa.

Chapisha Maoni

0 Maoni