Na.
Bakari S. Machumu- Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu
Hassan, ameagiza taasisi za umma kutathminiwa kwa kuzingatia tija ya
uwekezaji, ubora wa huduma, uwezo wa kujitegemea na mchango wake
katika uchumi wa Taifa.
Rais Dkt. Samia ameyasema hayo leo,
Ikulu Dar es Salaam, wakati wa hafla ya Siku ya Gawio 2026 iliyobeba
kaulimbiu isemayo, “Uwekezaji wa Umma wenye Matokeo: Nguzo ya
Uchumi Shindani na Maendeleo Endelevu kuelekea Dira 2050,” ambapo
amepokea gawio na michango yenye thamani ya shilingi trilioni 1.327
kutoka kwa mashirika, taasisi za umma na kampuni ambazo Serikali ina
hisa chache.
Amesema ongezeko la gawio la mwaka huu limetokana
na kuimarika kwa tija, uzalishaji na ufanisi wa taasisi za umma, huku
akisisitiza kuwa mafanikio ya taasisi hayapaswi kupimwa kwa gawio
pekee, bali pia kwa ubora wa huduma, uwezo wa kujitegemea na mchango
wake katika ukuaji wa uchumi.
Rais Dkt. Samia pia ameagiza
taasisi zilizoshindwa kutoa gawio, zilizotoa pungufu au zilizopunguza
kiwango cha gawio zikilinganishwa na mwaka uliopita kufanyiwa
tathmini ili kubaini sababu za mwenendo huo na kuchukua hatua
stahiki.
Aidha, amezitaka wizara, bodi na watendaji wakuu wa
taasisi za umma kusimamia kwa karibu utendaji wa taasisi zilizo chini
yao, akisisitiza kuwa uwajibikaji na tija si jukumu la Ofisi ya
Msajili wa Hazina pekee. Pia ameielekeza Ofisi hiyo kuendelea
kusimamia uwekezaji wa Serikali ili ulete manufaa yanayolingana na
thamani ya umiliki wa Serikali.
Akizungumzia Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2050, Rais Dkt. Samia amesema utekelezaji wake unahitaji
taasisi zenye nidhamu, uadilifu, ubunifu na utendaji unaopimwa kwa
matokeo badala ya mazoea.
“Hatutaweza kujenga uchumi
shindani kwa taasisi zinazofanya kazi kwa mazoea. Tunahitaji taasisi
zinazopimwa kwa matokeo badala ya takwimu pekee,” amesema Rais Dkt.
Samia.
Aidha, amezipongeza taasisi zilizoongeza gawio,
zilizorejea kwenye faida na zilizopunguza utegemezi wa ruzuku,
akisema hatua hiyo inaashiria kuimarika kwa utendaji wa taasisi za
umma.
Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na
Uwekezaji, Prof. Kitila Alexander Mkumbo, amesema mafanikio hayo
yanatokana na mageuzi ya kiuchumi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia
kupitia falsafa ya 4R na kuifungua nchi, hatua iliyoweka msingi imara
wa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Kwa upande
wake, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amesema taasisi 14
kati ya 308 zimetunukiwa kwa kufanya vizuri katika utoaji wa gawio na
michango kwa Mfuko Mkuu wa Serikali.
Katika hafla hiyo, Rais
Dkt. Samia pia alitunukiwa Tuzo Maalum ya “Kinara wa Mageuzi katika
Kuimarisha Mifumo ya Usimamizi wa Mashirika ya Umma kwa Maendeleo
Jumuishi na Ustawi wa Taifa – Gawio Day 2026,” kwa mchango wake
katika kuimarisha usimamizi wa uwekezaji wa umma na kuongeza tija ya
taasisi za Serikali.
TAARIFA KWA MHARIRI
Gawio na
michango ya mwaka huu imefikia shilingi trilioni 1.327 kutoka
shilingi trilioni 1.028 ya mwaka jana, sawa na ongezeko la asilimia
30.
Katika mashirika na kampuni za kibiashara, idadi ya
taasisi zilizotoa gawio la shilingi bilioni 10 na zaidi imeongezeka
kutoka sita hadi 10, huku jumla ya gawio ikiongezeka kutoka shilingi
bilioni 267 hadi bilioni 481.5. Vinara ni Twiga Minerals (shilingi
bilioni 221.9), NMB Bank (shilingi bilioni 96.9) na Airtel Tanzania
(shilingi bilioni 65.4).
Kwa taasisi zinazochangia Mfuko Mkuu
wa Serikali, idadi ya zilizochangia shilingi bilioni 10 na zaidi
imeongezeka kutoka saba hadi 11, huku michango ikiongezeka kutoka
shilingi bilioni 305 hadi bilioni 431.4. Vinara ni Mamlaka ya Bandari
Tanzania (TPA) (shilingi bilioni 205.5), Mamlaka ya Vitambulisho vya
Taifa (NIDA) (shilingi bilioni 61) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania
(TCRA) (shilingi bilioni 42.8).


0 Maoni