Rais Samia awataka Majaji kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewaapisha majaji wa Mahakama Kuu aliowateua hivi karibuni kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kuwaapisha majaji hao, Rais Dkt. Samia amewataka kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, uwajibikaji na uzalendo, huku wakitambua uzito wa dhamana waliyopewa ya kusimamia haki za wananchi na maslahi ya Taifa kwa ujumla.

Amesema uteuzi wa majaji katika ngazi hiyo ya juu ya Mahakama ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha mfumo wa utoaji haki nchini, ikiwemo kukabiliana na ongezeko la mashauri pamoja na mahitaji ya wananchi ya kupata haki kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia amesema Serikali itaendelea kuiwezesha Mahakama ili kuongeza ufanisi katika utoaji haki na kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kimahakama kwa wakati na kwa usawa.

Aidha, amewataka majaji hao kuzingatia maadili ya kazi, nidhamu na busara katika maamuzi yao ili kuendelea kulinda hadhi ya Mahakama pamoja na kuimarisha imani ya wananchi kwa mhimili huo wa utoaji haki.

Majaji walioapishwa ni Imani Daud Aboud, Rabia Hussein Mohamed, Yose Joseph Mlyambina, Immaculata Kajetan Banzi, Cyprian Phocas Mkeha, Yohane Bokobora Masara, Juliana Laurent Masabo, Abdi Shaaban Kagomba na Mzee Ibrahim Ibrahim.


Chapisha Maoni

0 Maoni