Mwenyekiti wa Jumuiya ya
Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), Sheikh Alhad Mussa Salum amesema
jumuiya hiyo inapinga kauli zilizotolewa na baadhi ya maseneta wa
Bunge la Marekani waliodai kuwa Tanzania si salama na kwamba kuna
vitendo vya ubaguzi wa kidini pamoja na baadhi ya waumini kutotendewa
haki.
Akizungumza jijini Dodoma wakati wa mkutano na waandishi
wa habari, Sheikh Alhad amesema madai hayo ni uzushi usiokuwa na
msingi na kwamba kauli hizo zina lengo la kuchochea migawanyiko na
kuvuruga amani iliyopo nchini. Amesisitiza kuwa Tanzania imeendelea
kuwa mfano wa mshikamano wa kidini kwa muda mrefu.
Kwa upande
wake, Katibu wa JMAT, Askofu Israel Maasa amesema kwa zaidi ya nusu karne
Watanzania wa dini zote wamekuwa wakiishi kwa amani, utulivu na
kuheshimiana bila kujali tofauti zao za kiimani.
Askofu Maasa
amesema JMAT, ambayo inawakutanisha viongozi wa madhehebu mbalimbali
ya dini za Kiislamu, Kikristo na nyinginezo, itaendelea kuhamasisha
maridhiano, mshikamano na umoja wa kitaifa ili kulinda amani ya
nchi.
Aidha, jumuiya hiyo imeeleza kuunga mkono juhudi za Rais
Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha haki, uwajibikaji na
maridhiano nchini, ikiwemo hatua ya kuunda Tume ya Uchunguzi pamoja
na Tume ya Kijinai kuhusu matukio ya kabla na baada ya Oktoba 29,
2025, kwa lengo la kuweka mazingira bora ya upatikanaji wa haki na
Katiba Mpya kama alivyoahidi.
#SisiNiWamoja


0 Maoni