Lazaro Nyalandu: Taifa Lahitaji Kuaminiana Kurejesha Utulivu

 

Baada ya kuwasilishwa kwa ripoti ya matukio ya vurugu ya Oktoba 29, 2025, wadau wa siasa na diplomasia wamesisitiza kuwa mustakabali wa taifa unapaswa kujengwa juu ya maridhiano na kuaminiana ili kurejesha imani ya wananchi na kudumisha utulivu wa nchi.

Akizungumza katika mahojiano na vyombo vya habari vya kimataifa hivi karibuni, Mshauri wa Rais wa Diplomasia, Lazaro Nyalandu, amesema kuwa jukumu la msingi la Serikali ni kulinda usalama wa wananchi wake wakati wote.

Ameeleza kuwa kauli za Samia Suluhu Hassan zinaonesha dhamira ya kweli ya kutafuta suluhu ya kudumu, huku akisisitiza kuwa msingi mkubwa wa kufanikisha hilo ni kujenga kuaminiana miongoni mwa pande zote.

Aidha, amebainisha kuwa Tume iliyoongozwa na Othman Chande imekamilisha kazi yake na kuwasilisha ripoti, ambayo imeweka wazi baadhi ya ukweli kuhusu changamoto zilizokuwa zikilikumba taifa pamoja na hatua zilizochukuliwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Nyalandu, ripoti hiyo imeonyesha ushahidi unaoeleza namna baadhi ya waandamanaji walivyoshiriki katika vurugu hizo, wakiwa na silaha mbalimbali ikiwemo bunduki na vilipuzi, huku wengine wakidaiwa kupata mafunzo maalum katika kambi tofauti.

Ameongeza kuwa kwa kuzingatia maelezo ya tume, matukio ya Oktoba 29, 2025 yalikuwa na viashiria vya kupangwa, hali iliyosababisha Serikali kuchukua hatua za haraka kulinda maisha ya wananchi, akibainisha kuwa ilikuwa siku yenye majonzi na changamoto kubwa kwa kila Mtanzania.

#UmojaWetuNdiyoNguvuYetu
#turidhiane


Chapisha Maoni

0 Maoni