Na. Joyce Ndunguru, Njombe
Waziri wa
Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) amewahimiza wananchi
wanaoishi pembezoni mwa Hifadhi ya Mpanga Kipengere kutunza hifadhi hiyo kwa
kuzingatia kuwa, takribani vijiji 96 vya Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali na
vijiji/miji vya Ilembula, Igawa na Igwachanya vinanufaika na miradi ya maji
ambayo chanzo chake ni ndani ya hifadhi ya Mpanga Kipengere.
Mhe. Dkt. Kijaji aliyasema hayo Disemba 17,2025,
alipotembelea Hifadhi ya Mpanga Kipengere iliyopo katika Mikoa ya Njombe na
Mbeya kwa lengo la kujionea jinsi shughuli za utalii zinavyofanyika, ikiwa ni
muendelezo wa ziara yake ya kikazi katika maeneo yanayosimamiwa na Mamlaka ya
Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA).
“Tusipohifadhi na kuitunza hifadhi yetu hii ya
Mpanga kipengere tutakosa maji lakini tutakosa manufaa mengine ya kijamii na
kiuchumi tunayopata kupitia hifadhi hii, hivyo niwaombe vijiji vyote
vilivyotuzunguka tuweze kuhifadhi kwa pamoja”, alisema Waziri Kijaji.
Sambamba na hilo, Waziri Kijaji aliisisitiza TAWA
kuendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuongeza fursa za uwekezaji na
mazao mbalimbali ya utalii katika Hifadhi hiyo.
“Tuje na vivutio vipya vya utalii vilivyomo ndani ya
hifadhi yetu , lakini pia tuwaite wawekezaji, tuwauzie fursa ili wawekeze
nasi,” aliongeza Waziri Kijaji.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maliasili na
Utalii, Mhe. Hamad Chande (Mb) aliwataka watanzania wanaoishi Mikoa ya Nyanda
za Juu Kusini kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo ukanda huu yakiwemo
Maporomoko maarufu ya maji ya Kimani yanayopatikana ndani ya Hifadhi ya Mpanga
Kipengere.
Naye, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Mlage
Yussuf Kabange alisema TAWA imeboresha miundombinu mbalimbali ya utalii na
utawala iliyopo ndani ya hifadhi ikiwemo ujenzi wa banda za watalii, kambi ya
watalii, ofisi, ujenzi madaraja pamoja na barabara.
Kuhusu mahusiano na jamii, Kamishna Kabange alisema
vijiji vinavyoizunguka vinanufaika na miradi ya maji ambayo chanzo chake ni
ndani ya hifadhi ya Mpanga Kipengere. Aidha, mito iliyopo ndani ya Hifadhi ya Mpanga
Kipengere ni vyanzo muhimu vya maji ya skimu za umwagiliaji za Igomelo,
Malangali, Wangama, Wangamiko na Imalilo ambazo zinanufaisha jamii moja kwa
moja.
Katika ziara hiyo ya kikazi, Waziri Kijaji
aliambatana na Naibu Waziri Wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, Naibu
Katibu Mkuu (Utalii), Nkoba Mabula na viongozi wengine wa Wizara ya Maliasili
na Utalii.
Hifadhi ya Mpanga Kipengere inayopatikana Mikoa ya
Njombe na Mbeya ni hifadhi iliyosheheni vivutio vingi likiwemo Maporomoko ya
Maji takribani 50 na uwanda uliosheheni maua ya kuvutia.

0 Maoni