Wananchi wa Shigela-Busega watakiwa kuchukua tahadhari dhidi ya fisi

 

Wananchi wa Kijiji cha Shigela, Wilaya ya Busega mkoani Simiyu wametakiwa kuwa waangalifu na kuchukua tahadhari dhidi ya fisi wanaoripotiwa kuvamia makazi ya watu na kuleta hofu katika jamii.

Rai hiyo imetolewa  Oktoba 6, 2025 na Afisa Uhifadhi kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Lusato Masinde, wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo ambapo timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, TAWA na Maafisa Wanyamapori wa Halmashauri inaendelea kutoa elimu ya uhifadhi mkoani humo ili kupunguza madhara yatokanayo na wanyamapori wakali na waharibifu.

 “Tuchukue tahadhari kubwa, hatuko salama kwa sababu katika mazingira yetu hawa wanyamapori wapo na kuna vichaka na mapango mengi,” amesisitiza  Masinde.

Ameongeza kuwa watoto ndio waathirika wakubwa wa mashambulizi ya fisi, hivyo wananchi wanapaswa kuwa makini na kuhakikisha wanawalinda ipasavyo, hasa wakati wa jioni na usiku.

Kwa upande wake, Afisa Maliasili wa Wilaya ya Busega, Jesca Mathias, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuwasaidia wananchi wanaokumbwa na changamoto za wanyamapori wakali na waharibifu, ikiwemo kulipa kifuta jasho na machozi kwa waathirika wa matukio hayo.

“Wananchi wanapaswa kutoa taarifa mapema kuhusu majeruhi, vifo au uharibifu wa mali unaotokana na wanyamapori. Fomu maalum za malipo zitajazwa na kupelekwa Wizara ya Maliasili na Utalii ili hatua za kifuta jasho zichukuliwe kwa wakati,” amesema Jesca.

Naye, Afisa Wanyamapori Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Nassoro Wawa, amebainisha kuwa Serikali imeanzisha mfumo wa kielektroniki wa kukusanya taarifa za wananchi wanaopata athari kutokana na mashambulizi au uharibifu wa wanyamapori wakali na waharibifu.

“Mfumo huu unarahisisha upatikanaji wa taarifa kwa wakati. Taarifa zitatumwa moja kwa moja kutoka uwandani kupitia maafisa wanyamapori, kilimo na mifugo, jambo litakaloharakisha mchakato wa malipo,” amesema Wawa.



Chapisha Maoni

0 Maoni