India yapiga marufuku dawa ya kikohozi baada ya vifo vya watoto tisa

 

Majimbo matatu ya India yamepiga marufuku matumizi ya dawa ya kikohozi baada ya watoto wasiopungua tisa kufariki dunia, wakidaiwa kufa kutokana na kutumia dawa hiyo, mamlaka zimesema.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Afya ya India, sampuli za dawa ya kikohozi aina ya Coldrif, inayotengenezwa na kampuni ya Sresan Pharma iliyoko Tamil Nadu, kusini mwa India, zilionyesha kuwa na kemikali aina ya diethylene glycol (DEG).

DEG ni kemikali hatari inayotumika viwandani, ambayo ni sumu kali na inaweza kusababisha madhara makubwa kiafya hata kwa kiasi kidogo inapotumiwa na binadamu.

“Tumeona kuwa sampuli hizo zina kiwango cha DEG kilichozidi kikomo kinachokubalika,” ilisema taarifa ya wizara hiyo.

Waziri Mkuu wa jimbo la Madhya Pradesh, Mohan Yadav, ambako ndiko vifo vingi vimeripotiwa, alisema: “Uuzaji wa dawa hii umepigwa marufuku kote katika jimbo la Madhya Pradesh.”

Marufuku hiyo imeungwa mkono pia na majimbo mengine mawili kufuatia tahadhari hiyo ya kiafya.

Dawa za kikohozi zinazozalishwa India zimekuwa zikitiliwa shaka katika miaka ya hivi karibuni, zikihusishwa na vifo duniani, vikiwemo vifo vya watoto 70 Gambia mwaka 2022.



Chapisha Maoni

0 Maoni