Rais samia awang’oa vigogo DART na UDART

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametengua uteuzi wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), Dkt. Athumani Kihamia, na kumteua Said Habibu Tunda kushika nafasi hiyo.

Katika mabadiliko hayo, Rais Dkt. Samia pia ametengua uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART), Bw. Waziri Kindamba, na kumteua Pius Andrew Ng'ingo kushika nafasi hiyo.

Mabadiliko hayo yanakuja wakati huduma ya mabasi ya mwendo kasi ikikumbwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ucheleweshaji wa huduma, msongamano wa abiria vituoni, pamoja na malalamiko ya mara kwa mara kutoka kwa watumiaji wa mfumo huo.

Wakati huo huo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewateua David Kafulila na Ramadhan Dau kuwa wenyeviti wa bodi za Wakala na Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka.

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dk Moses Kusiluka imesema Rais Samia amevunja Bodi za Wakala na Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka na kuwateua Dau na Kafulila kuwa wenyeviti wapya.

Taarifa hiyo imesema Kafulila ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri yaWakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART). Dau ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART).

Huduma ya mabasi yaendayo haraka imekuwa mojawapo ya miradi muhimu ya usafiri jijini Dar es Salaam, lakini kwa muda sasa imekuwa ikilalamikiwa kwa kukosa ufanisi unaotarajiwa, jambo ambalo limekuwa likiibua maswali kwa wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri.


Chapisha Maoni

0 Maoni