Sarkozy ahukumiwa miaka mitano jela sakata la fedha za Gaddafi

 

Rais wa zamani wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy, amehukumiwa kifungo cha miaka mitano jela baada ya kupatikana na hatia ya kula njama ya uhalifu katika kesi inayohusiana na kupokea fedha haramu mamilioni ya euro kutoka kwa aliyekuwa kiongozi wa Libya, hayati Kanali Muammar Gaddafi.

Uamuzi huo umetolewa Alhamisi na Mahakama ya Jinai ya Paris, ambayo hata hivyo ilimuondolea mashtaka mengine ya rushwa ya kupokea na ufadhili haramu wa kampeni za kisiasa.

Kwa mujibu wa hukumu hiyo, Sarkozy atalazimika kuanza kutumikia kifungo hicho mara moja, hata kama atakata rufaa, jambo ambalo tayari ametangaza kuwa atalifanya.

Akizungumza nje ya mahakama baada ya kusomwa kwa hukumu hiyo, Sarkozy mwenye umri wa miaka 70, alisema uamuzi huo ni “muhimu mno kwa utawala wa sheria”, na kusisitiza kuwa kesi hiyo ina nia ya kisiasa dhidi yake.

Sarkozy alihudumu kama Rais wa Ufaransa kati ya mwaka 2007 na 2012. Anadaiwa kupokea fedha haramu kutoka kwa Gaddafi kwa ajili ya kufadhili kampeni yake ya uchaguzi mwaka 2007.

Upande wa mashtaka ulidai kuwa Sarkozy aliahidi kumsaidia Gaddafi kusafisha taswira yake kuwa mtu asiyehitajika katika mataifa ya Magharibi, kama sharti la kupokea msaada huo wa kifedha.

Hukumu hiyo imekuwa pigo kubwa kwa rais huyo wa zamani, ambaye kwa miaka kadhaa amekuwa akikabiliwa na tuhuma mbalimbali za ukiukwaji wa sheria wakati wa uongozi wake.

Chapisha Maoni

0 Maoni