Rais Samia: Mambo makubwa yamefenyika

 

Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema chama hicho hakina mashaka katika kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, mwaka huu kwa sababu mambo mengi makubwa yamefanyika.

Ametoa kauli hiyo Septemba 18, 2025 akihutubia maelfu ya wananchi katika Viwanja vya Hamburu, Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja.

"CCM tuna ujasiri,kuja kwenu kuomba kura na ujasiri huu unatokana na kwamba tumefanya mambo makubwa," Dkt. Samia aliwaambia maelfu ya watu aliohudhuria mkutano huo.

Ameongeza: "Ndiyo maana tunakuja kwenu kwa kujiamini kuomba kura, mtuchague tena ili twende tufanye mambo makubwa zaidi kama alivyosema Dkt. Mwinyi."

Awali, mgombea urais wa Zanzibar na Rais wa visiwa hivyo, Dkt. Hussein Mwinyi alieleza mambo mengi makubwa yaliyofanywa na serikali yake pamoja na ushirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Dkt. Samia amesema wakipewa ridhaa, Serikali za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar zitaweka mazingira yatakayokuza kipato cha mwananchi mmoja mmoja.

Amesema moja ya ahadi ya CCM ni kuendelea kukuza uchumi na kipato cha mwananchi mmoja mmoja hatua ambayo itawezesha nchi kujitegemea.

"Katika kujenga taifa linalo jitegemea, hatutafika huko mpaka kila mtu ndani ya Tanzania yetu, kila kijana awe na shughuli inayompa kipato yeye mwenyewe asimame kama mtu mmoja, ajitegemee halafu kwa ujumla wetu tunaweza kujitegemea," alifafanua Dkt. Samia.

"Na hii ndio kazi tunayoiendea, tutakachokifanya ni kuandaa mazingira kwa vijana wetu kwa Watanzania kuweza kuwa na shughuli za kufanya, kuingiza kipato ili kila mmoja ainue ustawi wa maisha yake," alibainisha.

Ameongeza kuwa matokeo ya ukuaji uchumi na utekelezaji ahadi za CCM kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, umeonekana dhahiri uwezo wa Dkt. Mwinyi katika kuwaongoza Wazanzibari.

Ameeleza kuwa ukuaji uchumi kwa Tanzania Bara umeongezeka kwa asilimia sita huku Zanzibar ukiwa juu zaidi kwa asilimia 7.1 kwa mwaka.

"Zaidi uchumi umekuwa hata mifukoni kwa kila mwananchi. Wakati nilipokuwa nikiwasili Nungwi nilikuwa nikitazama kila pande na kujionea namna ambavyo kumejengeka nyumba nzuri za makazi, biashara zinafanyika na mambo yanaenda vyema kwa amani na utulivu," lisema Dkt. Samia.

Akizungumzia pia ukuaji wa sekta ya utalii Bara na Zanzibar, na kuwainua wananchi wa hali ya chini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Ameahidi kuendelea na utekelezaji wa miradi kupambana na mabadiliko ya tabianchi, na kuimarisha uchumi wa buluu hususani uvuvi katika bahari kuu na suala la mafuta na gesi.

Alisema pande mbili za Muungano zimeshirikiana kukuza uhusiano wa kidiplomasia na kukuza jina la Tanzania.

Na. Aboubakary Liongo- Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM

Chapisha Maoni

0 Maoni