Othman aanza ziara ya kukutana na wafuasi Pemba

 

Mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo, Othman Masoud Othman, ambaye pia alikuwa mgombea urais wa Zanzibar kupitia chama hicho, ameanza ziara maalum ya siku nne kisiwani Pemba yenye lengo la kuimarisha mshikamano wa wanachama na kufufua ari ya kisiasa ndani ya chama hicho.

Ziara hii, ambayo ni ya kwanza tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, imeanza kwa hamasa kubwa, huku maelfu ya wafuasi na wanachama wa ACT Wazalendo wakijitokeza kwa wingi kumpokea kiongozi wao katika ofisi za mratibu wa chama eneo la Gombani, wilaya ya Chake Chake.

Akihutubia wananchi katika mkutano huo, Othman Masoud alisema kuwa huu ni wakati wa Wazanzibari kusimama imara kwa umoja na mshikamano ili kulinda amani, utu na heshima ya Zanzibar.

Ameeleza kuwa chama chake kitaendelea kusimama kidete katika kudai uchaguzi huru, haki na ushirikishwaji wa kweli wa wananchi katika maamuzi yanayohusu mustakabali wa taifa.

Aliongeza kuwa, “Tunataka Zanzibar yenye uwazi, usawa na uadilifu. Tunataka demokrasia inayojengwa juu ya misingi ya heshima na haki kwa wote. Huu ndio urithi tunaoutaka kwa vizazi vijavyo.”

Othman pia alitumia fursa hiyo kuwashukuru wanachama wa ACT Wazalendo kwa kuendelea kuwa na imani na chama, akiwataka kuendeleza juhudi za kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa umoja, maendeleo na uadilifu wa kisiasa.

Ziara ya Othman Masoud inatarajiwa kuendelea katika mikoa yote minne ya kichama kisiwani Pemba, ambapo atakutana na viongozi, wanachama na wananchi kwa lengo la kusikiliza changamoto zao na kujadili mustakabali wa Zanzibar katika siasa za sasa.



Chapisha Maoni

0 Maoni