Dar yarejea kwenye amani, wafanyabiashara wasimulia machungu ya vurugu

 

Jiji la Dar es Salaam limerejea kwenye utulivu huku shughuli za kibiashara na kijamii zikipamba moto, baada ya kipindi kifupi cha mvutano kufuatia uchaguzi. Hata hivyo, athari za vurugu hizo bado ni kumbukumbu chungu kwa wafanyabiashara wengi, ambao wanashukuru kurudi kwa amani na kusisitiza umuhimu wa kulinda urithi huo wa kitaifa.

Mfanyabiashara Mzee Elia Moshi Afunguka Mmoja wa wafanyabiashara wakongwe, Elia Moshi, ametoa ushuhuda wake wa kile kilichotokea, akibainisha kuwa vurugu za hivi karibuni zilimwacha na majonzi makubwa.

"Uchumi wa wengi ni mdogo, wanategemea kutoka ndio wapate kula. Kilichotokea sitakisahau, kwani katika umri wangu huu mkubwa sijawahi kukiona Tanzania," alisema Moshi.

Moshi alisisitiza kuwa matukio hayo hayakuwa maandamano halisi, bali yalikuwa ni uvunjaji wa sheria uliotekelezwa na makundi ya wahalifu.

"Yale hayakuwa maandamano, yalikuwa ni uvunjaji wa sheria kwa kuharibu na kupora mali za watu binafsi na zile za umma. Maandamano yanajulikana, watu hueleza hasira zao kwa kupitia maneno, lakini sio vile. Makundi ya waporaji yalihusika na kuvunja amani," aliongeza kwa msisitizo.

Kama Bw. Moshi, wafanyabiashara wengi wameathirika moja kwa moja na machafuko hayo, hasa wale wanaotegemea kipato cha kila siku.

Maandamano na vurugu za muda mfupi ziliwarudisha nyuma wafanyabiashara wengi kibiashara, hasa wale wadogo ambao hutegemea mtaji mdogo na mzunguko wa haraka.

Baada ya kurejea kwa amani, wafanyabiashara sasa wanatoa wito wa "Kazi na Utu," wakisisitiza kuwa biashara ziendelee tu na kwamba ni muhimu "Maisha yaendelee sasa."

Kwa pamoja, wananchi wa Dar es Salaam wanakubaliana kwamba amani ni msingi wa maisha na maendeleo yao, na haipaswi kuchezewa.

Chapisha Maoni

0 Maoni