AG: Mawakili wa Serikali tumieni maarifa ya hifadhi ya jamii kulinda haki za wanachama

 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari, amewataka Mawakili wa Serikali kuyatumia maarifa wanayoyapata kupitia mafunzo ya Hifadhi ya Jamii ili kuhakikisha kuwa sheria na kanuni za hifadhi ya jamii zinatekelezwa kwa ufanisi na kulinda haki na maslahi ya wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii nchini.

Mhe. Johari ametoa wito huo Septemba 18, 2025, wakati akifungua mafunzo ya siku mbili kuhusu Hifadhi ya Jamii kwa Mawakili wa Serikali yaliyoandaliwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mwanasheria Mkuu amesema kuwa mafunzo hayo yatakuwa chachu ya kuongeza ujuzi kwa Mawakili wa Serikali katika maeneo mbalimbali ya kisheria, hususan yanayohusiana na Hifadhi ya Jamii. Alizitaja baadhi ya sheria hizo kuwa ni pamoja na Sheria ya Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma [Sura ya 371], Sheria ya Mikataba [Sura ya 345], Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini [Sura ya 366], pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Fedha na Uwekezaji.

“Ni matarajio yangu kuwa mafunzo haya yatajikita katika maeneo muhimu ya kisheria na kiutawala, ikiwemo muundo wa kisheria wa PSSSF, majukumu yake ya msingi, pamoja na haki na wajibu wa wanachama, wastaafu na wategemezi wao,” amesema Mhe. Johari.

Aidha, Mwanasheria Mkuu amebainisha kuwa mafunzo hayo yatawasaidia Mawakili wa Serikali kuwa na uelewa mpana wa namna ya kushughulikia masuala ya kisheria yanayohusu Mfuko wa PSSSF kwa kutumia mbinu za usuluhishi na majadiliano, badala ya kusubiri migogoro ifikishwe mahakamani.

“Mbali na kupunguza mashauri yasiyo ya lazima, mafunzo haya pia yatawezesha kuwekwa kwa misingi imara ya kisheria katika utekelezaji wa shughuli za kila siku za Mfuko, pamoja na kuimarisha uhusiano kati ya PSSSF na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa manufaa ya Taifa,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Johari amewataka Mawakili wa Serikali wanaoshiriki mafunzo hayo kuwa na ari ya kujifunza na kuhakikisha kuwa maarifa wanayoyapata yanatumika kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

“Tunapozungumzia hifadhi ya jamii, tunazungumzia maisha ya watumishi kabla na baada ya kustaafu. Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa mifumo hiyo inalindwa kwa mujibu wa sheria,” amesisitiza.

Mafunzo hayo yanaendelea kwa siku mbili na yanatarajiwa kuongeza tija katika usimamizi wa masuala ya hifadhi ya jamii nchini. 



               

Chapisha Maoni

0 Maoni