Mamlaka
ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya utalii,
imeadhimisha Siku ya Utalii Duniani kwa kuhamasisha utalii wa kupanda milima
kupitia Mlima Lomalasin, uliopo ndani ya eneo la hifadhi hiyo maarufu duniani.
Maadhimisho
hayo yaliyofanyika jana Septemba 27, 2025, yamelenga kutangaza vivutio vya
utalii wa asili vinavyopatikana ndani ya Ngorongoro, huku Mlima Lomalasin
ukielezwa kuwa moja ya vivutio vinavyoibukia kwa kasi katika eneo hilo.
Mlima huo
unaotajwa kuwa wa tatu kwa urefu nchini Tanzania, una urefu wa mita 3,682
kutoka usawa wa bahari na umekuwa kivutio kikubwa kwa watalii wanaopenda utalii
wa milima kutokana na mandhari yake ya kuvutia na mazingira asilia
yaliyohifadhiwa vyema.
Akizungumza
wakati wa shughuli ya kupanda mlima huo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi
anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko NCAA, Mariam Kobelo, alisema maadhimisho
ya mwaka huu yamelenga kuhamasisha utalii wa ndani kupitia mazao mbadala ya
utalii.
"Leo
tunapoadhimisha Siku ya Utalii Duniani, tunatumia fursa hii kutangaza Mlima
Lomalasin na kuhamasisha Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki katika
utalii wa kupanda milima. Huu ni mlima wa kipekee unaotoa fursa ya kuona
mandhari nzuri ya asili, sambamba na kuutangaza utalii wa kiikolojia,"
alisema Kobelo.
Kwa
upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya Utalii ya Land Africa Safaris, Bw.
Timothy Mdinka, alisema Mlima Lomalasin una upekee wa kipekee kijiografia na
kwamba umeendelea kuwavutia wageni kutoka mataifa mbalimbali duniani.
"Mlima
huu upo katika eneo la kipekee kijiolojia linalounganisha vivutio vingine
muhimu kama Kreta ya Empakai, Kreta ya Olmoti, Mlima Losirwa, Oldoinyo Lengai
na eneo la kihistoria la Engaruka. Hii inaufanya kuwa kivutio cha kipekee kwa
watalii wa ndani na wa kimataifa," alisema Mdinka.
Siku ya
Utalii Duniani huadhimishwa kila mwaka Septemba 27 kwa lengo la kuhamasisha
maendeleo ya utalii endelevu na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango wa
sekta hiyo katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Kaulimbiu ya
mwaka huu ni "Utalii na Mageuzi Endelevu."
Maadhimisho
hayo yamehudhuriwa na wadau mbalimbali wa utalii wakiwemo wawakilishi kutoka
Wizara ya Maliasili na Utalii, Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, kampuni za
utalii ikiwemo Land Africa Safaris, Asante Tours, Crater Lodge, Azam TV, Nols
& Beyond pamoja na wakazi wa Kijiji cha Bulati ambacho kimebarikiwa kuwa
mwenyeji wa Mlima Lomalasin.




0 Maoni