Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu), Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, ameipongeza Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa mafanikio makubwa katika kuboresha utendaji wa mashirika ya umma nchini.
Akizungumza Ijumaa,
Julai 4, 2025, wakati wa ziara yake katika banda namba 39 (Ukumbi wa
Kilimanjaro) kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam
(Sabasaba), Mhe. Kikwete alisema mageuzi hayo yamechangia mashirika mengi ya
umma kujiendesha kwa ufanisi na kutoa mchango mkubwa kwa Serikali.
"Tunaishukuru
Ofisi ya Msajili wa Hazina chini ya uongozi imara wa Bw. Nehemiah Mchechu kwa
kuwezesha taasisi za umma kuongeza ufanisi wao," alisema Mhe. Kikwete.
Akiweka mkazo juu ya
mafanikio hayo, Mhe. Kikwete alieleza kuwa mageuzi hayo ni sehemu ya dhamira ya
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha
utendaji katika sekta ya umma.
"Wote ni
mashahidi, tumeona mabadiliko makubwa ya kiutendaji katika taasisi za umma,
hali ambayo haikuwahi kushuhudiwa miaka ya nyuma," alisema.
Kwa mujibu wa taarifa
zilizotolewa, mashirika kadhaa ambayo awali yalikuwa yanapata hasara sasa
yameimarika kifedha na kuanza kutoa gawio kwa Serikali. Miongoni mwa mashirika
hayo ni pamoja na OSHA, ambalo kwa mwaka wa fedha 2024/25 limechangia Shilingi
bilioni 10.5 kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali.
Mashirika mengine
yaliyotajwa kuonesha ufanisi mkubwa ni Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO),
Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), na Shirika la Madini la Taifa
(STAMICO).
Akitoa mfano wa
mafanikio hayo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma katika
Ofisi ya Msajili wa Hazina, Bw. Sabato Kosuri, alisema ufanisi umeongezeka kwa
kiwango kikubwa kwenye Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA).
"Kwa mwaka wa
fedha uliopita, Mamlaka ya Bandari imeongeza mchango wake kwenye Mfuko Mkuu wa
Serikali kutoka Shilingi bilioni 155.7 mwaka 2023/24 hadi Shilingi bilioni 181
mwaka 2024/25," alisema Bw. Kosuri.
Aidha, matumizi ya
kawaida kwa ajili ya uendeshaji wa bandari yamepungua kwa kiasi cha Shilingi
bilioni 505.59, ikiwa ni ufanisi wa asilimia 46.
Waziri Kikwete
aliihakikishia Ofisi ya Msajili wa Hazina kuwa Serikali itaendelea kuiunga
mkono katika jitihada zake za kuimarisha taasisi za umma.
“Endeleeni kufanya
kazi kwa bidii. Pale ambapo kuna mambo yanayohitaji kubadilishwa katika taasisi
zilizo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, hesabuni mmepata ushirikiano kutoka
kwetu,” alisema.
Maonesho ya Sabasaba
mwaka huu yamehudhuriwa na taasisi mbalimbali za umma na binafsi, zikiwa na
lengo la kuonesha mafanikio na huduma wanazotoa kwa wananchi, sambamba na
kukuza ushirikiano wa kibiashara.
0 Maoni