UNDP, TFS watembelea Lake Duluti kujionea maboresho ya uhifadhi na utalii

 

Ujumbe wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) ukiongozwa na Mwakilishi Mkazi, Shigeki Komatsubara, kwa kushirikiana na ujumbe wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ukiongozwa na Kamishna wa Uhifadhi, Prof. Dos Santos Silayo, umetembelea Hifadhi ya Msitu wa Mazingira Asilia wa Ziwa Duluti jana Julai 23, 2025.

Ziara hiyo imelenga kujionea maendeleo ya maboresho katika uhifadhi na miundombinu ya utalii, ambayo inalenga kuvutia wageni zaidi katika hifadhi za misitu ya asili nchini.

UNDP ni mshirika mkuu wa utekelezaji wa mradi wa kitaifa unaoitwa “Kujenga Ustahimilivu wa Bioanuwai ya Misitu Dhidi ya Matishio ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi katika Hifadhi za Misitu ya Mazingira Asilia Tanzania”.

Mradi huo wa miaka sita, wenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 15, unafadhiliwa na Mfuko wa Mazingira Duniani (GEF) kupitia UNDP na unatekelezwa kwa kushirikiana na TFS katika hifadhi mbalimbali za misitu ya mazingira asilia.

Umezinduliwa rasmi mapema mwaka huu na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana, katika Msitu wa Pugu-Kazimzumbwi, mkoani Pwani.

Lengo kuu la mradi huo ni kuimarisha ustahimilivu wa bioanuwai ya misitu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi, huku ukichangia maendeleo endelevu ya jamii zinazozunguka hifadhi hizo.

Ziara ya Duluti imefuatia Mkutano wa Tatu wa Kamati ya Uendeshaji wa Mradi, uliofanyika Julai 22, 2025 katika Ukumbi wa Ngorongoro, Arusha, ambapo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba, aliongoza kama Mwenyekiti wa kikao hicho.



Chapisha Maoni

0 Maoni