TEF yampa kongole Ernest Sungura kwa kuteuliwa nafasi za Kimataifa

 

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limempongeza Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Ndugu Ernest Sungura, kwa kuchaguliwa kushika nafasi mbili muhimu za kimataifa katika sekta ya habari.

Sungura ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mabaraza ya Habari Duniani (WAPC), pia  Makamu Mwenyekiti wa Mabaraza ya Habari ya Afrika Mashariki (EAPC), hatua ambayo TEF imeielezea kuwa ni heshima kwa taifa na tasnia ya habari kwa ujumla.

Akitoa pongezi hizo leo kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile alisema kuwa uteuzi huo si tu unamtambulisha Sungura kimataifa, bali pia unaonesha jinsi Tanzania inavyoendelea kutoa mchango mkubwa katika kukuza na kulinda taaluma ya habari duniani.

“TEF inatambua juhudi na uongozi mahiri wa Ndugu Sungura, ambao umejenga misingi imara ya ushirikiano wa kikanda na kimataifa kupitia Mtandao wa Mabaraza Huru ya Habari Afrika (NIMCA), na sasa ameendelea kupanda hadi ngazi ya WAPC,” alisema Balile.

Aliongeza kuwa mchango wa Sungura katika kuimarisha mazingira wezeshi ya uhuru wa habari, uwajibikaji, na weledi katika sekta ya habari umekuwa wa kuigwa, na sasa dunia inatambua juhudi hizo.

“Tunamtakia kila la heri katika majukumu yake mapya ya kimataifa, na tunamhakikishia kuwa TEF itaendelea kushirikiana naye kwa karibu kwa maendeleo ya tasnia ya habari nchini na duniani kote,” alisema Balile.

Uteuzi huo unakuja wakati ambapo sekta ya habari inaendelea kukabiliana na changamoto mbalimbali zikiwamo za kiuchumi, huku mchango wa viongozi kama Sungura ukihitajika zaidi katika kuimarisha maadili, uwazi na uhuru wa vyombo vya habari.

Chapisha Maoni

0 Maoni