CCM Yahairisha Uteuzi wa Mwisho wa Wagombea hadi Julai 28

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza kusogeza mbele tarehe ya uteuzi wa mwisho wa wagombea wake wa nafasi za Ubunge na Udiwani kutoka Julai 19 hadi Julai 28, 2025.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 19, 2025, jijini Dodoma, Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa chama hicho, Ndg. Amos Makalla amesema kuwa mchakato wa ndani unaendelea vizuri huku uchambuzi wa majina ya wagombea ukifanyika kwa umakini mkubwa.

“Maandalizi ya mchakato wa uchaguzi ndani ya CCM yanaendelea vizuri. Kikao cha mwisho cha uteuzi wa wagombea sasa kimepangwa kufanyika Julai 28, 2025 hapa Dodoma, badala ya leo Julai 19, 2025. Wagombea ni wengi sana, kazi ya kuchambua ni kubwa, na sisi tunataka tufanye kwa umakini,” alisema Makalla.

Amesema chama hicho kimeongeza muda wa mchakato huo ili kuhakikisha kuwa kila hatua ya uchambuzi wa wagombea inafanyika kwa makini na kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na chama, “Wagombea wa relax (watulie) wakati tunaendelea na mchakato.”

Hatua hiyo ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu, ambapo CCM kama chama tawala kinaendelea na mchakato wa kuwapata wagombea wake watakaopeperusha bendera ya chama hicho katika nafasi mbalimbali za uongozi.

Uamuzi huo unakuja wakati ambapo macho ya wanachama na wananchi kwa ujumla yameelekezwa kwa CCM, wakisubiri kwa hamu majina ya watakaochuana katika kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Chapisha Maoni

0 Maoni