Rostam Azizi: Tuanzishe Mfuko wa Maendeleo ya Vipaji

 

Mfanyabiashara maarufu nchini, Bw. Rostam Azizi, ametoa wito kwa Serikali kuwekeza kwa makusudi katika rasilimali watu, hususan vijana, ili kuiwezesha Tanzania kupiga hatua kubwa za maendeleo katika karne ya 21.

Akitoa maoni yake jana katika hafla ya uzinduzi wa Dira 2050,  Bw. Azizi alisema hatua ya kwanza ni kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vipaji wenye bajeti ya takriban Dola za Kimarekani milioni 70 kila mwaka kwa kipindi cha miaka kadhaa, ili kuwajengea uwezo vijana takribani 1,000 katika nyanja za kimkakati kama vile Uhandisi, Akili Bandia (AI), Sayansi ya Takwimu, Fedha, pamoja na kozi nyingine zitakazotambuliwa kulingana na mahitaji ya taifa.

“Kupitia mpango huu, tutawapeleka vijana wetu kusoma katika vyuo bora duniani kama vile vilivyoko Marekani, Uingereza na China, kisha warejee kuja kuhudumu katika taasisi za serikali kwa mkataba maalum,” alisema.

Aidha, alisisitiza kuwa mpango huo si wa masomo pekee bali ni uwekezaji wa kimkakati katika wasanifu wa mwelekeo mpya wa taifa kama ulivyoainishwa kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Vyuo vya Ndani Navyo Vipewe Kipaumbele

Hata hivyo, Bw. Azizi alisisitiza kuwa nchi haiwezi kusubiri mpaka vijana walioko nje warejee ndipo hatua zichukuliwe. Alitaka vyuo vya ndani viimarishwe, mitaala iboreshwe, utafiti uongezwe, na mfumo wa elimu uendane na mahitaji ya sasa ya kiuchumi.

“Tunapaswa kuhakikisha vyuo vyetu vina uwezo wa kuzalisha wataalamu wa viwango vya kimataifa. Hatuna budi kuboresha mfumo wetu wa elimu kutoka ndani,” alisema.

Viongozi Pia Wapate Mafunzo ya Kimataifa

Katika hoja nyingine, Bw. Azizi alipendekeza kuwa viongozi waliopo katika taasisi mbalimbali za umma wapewe fursa ya kushiriki katika programu za uongozi za kimataifa, ili kuwajengea uwezo wa kuongoza katika mazingira mapya.

“Hii itawasaidia kuvitumia vizuri vipaji vipya vitakavyoibuka,” aliongeza.

Balozi Watambue Watanzania Wenye Ujuzi Ughaibuni

Kama hatua ya dharura, aliishauri Serikali kupitia balozi zake kuwatambua na kuwarudisha nyumbani Watanzania walioko nje wanaosomea au kufanya kazi katika nyanja muhimu, ili taifa linufaike na maarifa yao.

“Kwa bahati nzuri tuna Waziri wa Mambo ya Nje, Mhe. Mahmood Thabit, ambaye anaamini sana katika kutumia diplomasia kwa maendeleo ya uchumi wa nchi – mimi humuita Waziri wa Diplomasi ya Uchumi,” alisema kwa msisitizo.

Sekta Binafsi na Viwanda Vilindwe

Katika hitimisho lake, Bw. Azizi alisisitiza umuhimu wa Serikali kuilinda sekta binafsi ya ndani, hasa viwanda, ikiwa taifa linakusudia kufikia uchumi wa dola trilioni moja.

“Tunakushukuru Mheshimiwa Rais kwa jitihada zako za kuwavutia wawekezaji wa nje, lakini mwisho wa siku Watanzania ndiyo watakaolijenga taifa lao. Tunapaswa kuwawekea mazingira rafiki na ya ulinzi wawekezaji wa ndani,” alisema.

Alionya kuwa hakuna nchi duniani iliyoweza kufanikisha mapinduzi ya viwanda bila kulinda viwanda vyake vya ndani.

“Serikali izingatie hili tunapojiandaa kutekeleza Dira 2050,” alihitimisha.

Chapisha Maoni

0 Maoni