Neema Mbuja aking’arisha Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Nishati Osaka

 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, amemkabidhi tuzo ya umahiri Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Nishati, Bi. Neema Chalila Mbuja, kutokana na mchango wake mkubwa katika sekta ya mawasiliano wakati wa Maonesho ya Dunia ya Biashara ya Osaka, Japan.

Makabidhiano hayo yalifanyika jana Julai 13, 2025, wakati wa kilele cha Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, maarufu kama Sabasaba, yaliyofanyika katika viwanja vya Mwalimu Nyerere.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Majaliwa alimtaja Bi. Mbuja kuwa ni miongoni mwa watumishi wa umma waliotoa mchango wa kipekee katika kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia mawasiliano ya kisasa, hasa kwenye maonesho ya Osaka Expo 2025.

“Bi. Mbuja ameonyesha weledi mkubwa katika kuwasilisha na kutangaza fursa za Tanzania kwenye jukwaa la kimataifa. Amefanya kazi kubwa ya kuitangaza nchi yetu na Wizara ya Nishati kwa ujumla,” alisema Majaliwa.

Kwa upande wake, Bi. Mbuja alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutambua juhudi zake na kutoa tuzo hiyo, ambayo ilitolewa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE). Aliahidi kuendelea kuitangaza Tanzania kupitia Wizara ya Nishati katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa.

Tuzo hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kutambua na kuthamini watumishi wa umma wanaofanya kazi kwa weledi na uzalendo katika kuiwakilisha vyema Tanzania nje ya mipaka.


Chapisha Maoni

0 Maoni