Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Nurdin Babu, amesema Mwenge wa Uhuru umekimbizwa kwa umbali wa kilomita 895 katika mkoa huo na kukagua jumla ya miradi 52 yenye thamani ya zaidi ya Shilingi Bilioni 84.
Mhe. Babu alitoa
taarifa hiyo leo Julai 5, 2025 wakati wa hafla ya makabidhiano ya Mwenge wa
Uhuru kwa Mkoa wa Arusha, iliyofanyika katika kijiji cha Kingori, kata ya
Malula, wilayani Arumeru.
Amesema kuwa katika
ziara hiyo ya Mwenge, miradi 22 ilizinduliwa rasmi, 20 iliwekewa mawe ya msingi
huku mingine 10 ikitembelewa na kukaguliwa. Kwa mujibu wake, miradi yote hiyo
imeridhiwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa.
Ameongeza kuwa Mwenge
huo pia ulipitia miradi tisa ya kijamii ikiwa ni sehemu ya kuonesha mshikamano
na ushirikiano baina ya sekta binafsi na Serikali ya Mkoa wa Kilimanjaro katika
kuharakisha maendeleo ya wananchi.
Katika kukabiliana na
athari za mabadiliko ya tabianchi, Mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa jumla ya
mitungi 370 ya gesi safi ya kupikia imetolewa kwa wananchi wa maeneo
mbalimbali, ikiwa na thamani ya zaidi ya Shilingi Milioni 18.4, kama sehemu ya
jitihada za kupunguza matumizi ya kuni na mkaa.
Kwa upande wake,
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Bw. Ismail Ali Ussi, alipongeza
utekelezaji wa miradi hiyo, akisema imefanyika kwa ubunifu, tija na ufanisi
mkubwa na inaakisi thamani halisi ya uwekezaji wa fedha za umma.
“Nimevutiwa na
utendaji kazi wa Wakuu wa Wilaya katika Mkoa huu. Kama ningekuwa na mamlaka ya
ushauri, ningeshauri wasiondoke hapa. Waendelee kumsaidia Mheshimiwa Rais, Dkt.
Samia Suluhu Hassan, kusimamia maendeleo ya wananchi,” alisema Ussi.
Mwenge wa Uhuru
unatarajiwa kuendelea na mbio zake mkoani Arusha, ambapo utazindua na kukagua
miradi mbalimbali ya maendeleo kama ilivyo desturi ya mbio hizo zinazobeba
ujumbe wa kitaifa kila mwaka.
0 Maoni