Mhifadhi mstaafu
aliyewahi kuwa Mhifadhi Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Ugani na Uenezi wa Wakala
wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Charles Ngatigwa, leo Juni 3, 2025, ameonesha
kufurahishwa na hatua kubwa za maboresho zinazofanywa na TFS katika Maonesho ya
48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).
Ngatigwa, ambaye
alitembelea banda la TFS mapema leo akiwa ameongozana na wajukuu zake, amesema
ameshangazwa na kufurahishwa kuona mabadiliko makubwa kuanzia muonekano wa
banda hadi huduma za ubunifu zinazotolewa, ambazo zimeendelea kuhamasisha
wananchi wengi zaidi kutembelea na kujifunza.
“Kweli nimeona
mapinduzi makubwa sana. Kipindi nikiwa kwenye utumishi tulikuwa na changamoto
nyingi za uhamasishaji na elimu, lakini leo hii nimejionea mwenyewe jinsi TFS
inavyotumia fursa ya Sabasaba kufundisha na kutoa huduma kwa vitendo. Hii ni
hatua kubwa na ya kupongezwa,” amesema Ngatigwa.
Wajukuu zake
walivutiwa zaidi na shamba darasa la ufugaji nyuki lililoandaliwa na TFS ndani
ya banda hilo, na kufikia hatua ya kuomba wafundishwe hatua kwa hatua jinsi ya
kufuga nyuki na kupata mazao yake.
Mhifadhi
anayeshughulikia Dawati la Nyuki TFS, Said Abubakar, alitumia muda huo kuwapa mafunzo
ya moja kwa moja kuhusu mnyororo mzima wa thamani wa ufugaji nyuki kuanzia
maandalizi ya mizinga, tabia za nyuki, ukusanyaji wa asali na bidhaa zingine
zinazotokana na nyuki.
Mbali na kujifunza,
vijana hao pia walipata fursa ya kuonja asali safi na kushuhudia jinsi nyuki
wanavyofanya kazi. Aidha, kama sehemu ya huduma maalum ya api-therapy
inayotolewa bandani hapo, waliruhusiwa kudungwa na nyuki kwa lengo la kujionea
manufaa ya tiba hiyo asilia inayozidi kupata umaarufu duniani.
Wote walikiri kufurahia
huduma hiyo na kuahidi kurudi tena kujifunza zaidi na kufuatilia fursa za
kuanzisha miradi midogo ya nyuki majumbani mwao.
Ngatigwa ametoa wito
kwa wananchi kutumia fursa ya Sabasaba kutembelea banda la TFS ili kujifunza
masuala mbalimbali yahusuyo uhifadhi, fursa za uwekezaji kwenye sekta ya misitu
na nyuki, pamoja na huduma nyingine za kitaalamu.
“Mtu yeyote anaweza
kupata fursa ya kutundika mizinga kwenye misitu iliyohifadhiwa bure kabisa na
kupewa elimu ya ufugaji na wataalamu wa TFS bila gharama yoyote. Hii ni hazina
kubwa, wananchi wengi hawajui,” amesema Ngatigwa.
Aidha, amewahimiza
wananchi wanaopenda kutumia asali kama tiba lishe kuhakikisha wanapita katika
duka maalum la Misitu Honey Shop lililopo ndani ya banda la TFS ili kupata
asali safi, salama na yenye viwango vya ubora vilivyohakikishwa.
TFS itaendelea kutoa
huduma na mafunzo hayo kwa wananchi katika viwanja vya Sabasaba hadi Juni
13, 2025.
0 Maoni