Balozi Tembele akutana na Ujumbe wa Wataalamu wa Wizara ya Fedha na PURA

 

Mheshimiwa Macocha M. Tembele, Balozi wa Tanzania nchini Indonesia amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha na Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) uliopo ziarani nchini Indonesia. Mazungumzo hayo yamefanyika mapema leo katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania- Jakarta.

Katika mazungumzo yake, Mheshimiwa Balozi aliueleza ujumbe huo kuhusu hatua kubwa ya maendeleo iliyofikiwa na Indonesia katika sekta ya mafuta na gesi na kuwataka kutumia vyema fursa ya ziara hiyo ili kupata uzoefu utakaoinufaisha Tanzania katika eneo la udhibiti na usimamizi wa shughuli za mkondo wa juu katika utafutaji, uendelezaji na uzalishashaji wa mafuta na gesi.

Kwa upande wake Dr. Remidius Ruhinduka, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha alimshukuru Mheshimiwa Balozi kwa uratibu wa ziara pamoja na mapokezi mazuri waliyopata na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yake ipasavyo.

Ujumbe huo upo ziarani nchini Indonesia kwa lengo la kujifunza na kupata uzoefu zaidi utakaowezesha kufanikisha uandaaji wa kanzidata ya msingi wa bei na gharama za uendeshaji wa shughuli za mkondo wa juu wa petroli Tanzania ambayo itaisasaidia nchi yetu kwenye majadiliano ya mikataba ya ugawanyaji wa mapato (PSA).



Chapisha Maoni

0 Maoni