Mwenge wa Uhuru ni alama ya Uhuru, Umoja na Maendeleo ya nchi yetu

 

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Stergomena Lawrence Tax (Mb) amesema, Mwenge wa Uhuru umepandishwa katika kilele cha Mlima Kilimanjaro kusherekea Miaka 60 ya historia yetu na kutukumbusha wajibu wetu wa kuhifadhi uhuru tulio nao kwa kujenga Taifa lenye umoja, mshikamano, nguvu na maendeleo.

Mhe. Dkt. Stergomena, amesema hayo leo tarehe 21, Oktoba 2024 katika hafla iliyofanyika Makao Makuu ya Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro, wakati wa mapokezi ya kikosi maalumu cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kilichopandisha Mwenge wa uhuru pamoja na bendera ya Taifa katika kilele cha Mlima Kilimanjaro.

Mhe. Dkt. Stergomena amenukuliwa akisema, "Mwenge wa uhuru si tu alama ya ukombozi bali pia ni kielelezo cha dhamira yetu kama nchi ya kuendelea kupigania amani, umoja na maendeleo ya nchi yetu."

Akitoa pongezi kwa Jeshi la Wananchi (JWTZ), Mkuu wa Jeshi la Ulinzi (CDF) Jenerali Jacob Mkunda, amekipongeza kikosi hicho maalumu  kilichopandisha Mwenge wa Uhuru pamoja na Bendera ya Taifa katika Mlima Kilimanjaro kwa weledi, uaminifu na uangalifu mkubwa wakiongozwa na Luteni Kanali Khalid Hamisi Khalid.

CDF Mkunda aliongeza, "Shukrani za dhati ziwaendee uongozi wa Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kwa ushirikiano mkubwa na ukarimu kwa timu nzima iliyopeleka Mwenge wa Uhuru na Bendera ya Taifa katika kilele cha Mlima Kilimanjaro."

Ikumbukwe kuwa tarehe 14, Oktoba 2024 Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Rais Samia Suluhu Hassan alimkabidhi Mwenge wa Uhuru na Bendera ya Taifa Mkuu wa Jeshi la Ulinzi Jenerali Jacob Mkunda, ili Jeshi hilo liupeleke kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro ikiwa ni sehemu ya sherehe za miaka 60 tangu kuanzishwa kwa mbio hizo za mwenge mwaka 1964.

Ambapo tarehe 15, Oktoba 2024  Kikosi maalumu cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kilianza safari ya kupandisha Mwenge wa Uhuru na Bendera ya Taifa katika kilele cha Mlima Kilimanjaro kutekeleza agizo hilo na safari hiyo kuhitimishwa rasmi leo tarehe 21, Oktoba 2024 kwa wanajeshi hao kurejea salama na wakiwa na furaha isiyo na kitabı.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali akiwemo, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA, watendaji wa taasisi za serikali, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa pamoja na viongozi wa Dini.

   Na. Happiness Sam - Kilimanjaro

Chapisha Maoni

0 Maoni