Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amewashukuru
wadau wa madini, wachimbaji wakubwa, wa kati, wadogo na wafanyabiashara ya madini
kwa kufikia muafaka wa kuwezesha utekelezaji wa kifungu cha 59 cha Sheria ya
Madini juu ya kutenga 20% ya uzalishaji wa dhahabu kwa ajili ya akiba ya nchi
kupitia BoT.
Mhe. Mavunde amesema kwamba muafaka
huyo umefikiwa katika kikao cha pamoja kati ya wadau wa madini na Benki Kuu ya
Tanzania (BoT) na Wizara ya Madini. “Tumefikia muafaka katika maeneo mengi na
hivyo kuwezesha utekelezaji wa sheria hiyo.”
Akiongea leo Oktoba 7, 2024 Waziri
Mavunde ametaja mambo muhimu waliofikia muafaka na wadau wa madini kuwa ni pamoja na bei
itakayotumika ni bei ya dhahabu duniani kama inavyotolewa na Tume ya Madini. Bei
hiyo hubadilika kila siku.
Pia, kufanyika kwa malipo ya asilimia
100 baada ya kupokea ripoti ya uchenjuaji wa dhahabu, ambapo muda wa malipo ni
ndani ya saa 24 baada ya kupata ripoti ya uchenjuaji.
Kwa maana hiyo chini ya utaratibu huu
wa malipo kwa miamala ya tarehe 02 Oktoba 2024, yalifanyika ndani ya masaa
sita, amesema Waziri Mavunde.
Hali kadhalika, kwa upande wa gharama
za kuchenjua dhahabu, Mhe. Mavunde ameeleza kuwa wamekubaliana Benki Kuu ya
Tanzania italipia asilimia 100 ya gharama za kuchenjua dhahabu.
Mhe. Mavunde amefafanua kuwa kifungu
cha 59 cha Sheria ya Madini juu ya kutenga 20% ya uzalishaji wa dhahabu kwa
ajili ya akiba ya nchi kupitia BoT kinamhusu mmiliki wa leseni ya chimbaji wa
madini na mfanyabiashara mkubwa wa madini.
“Wafanyabiashara watapata motisha ya mrabaha
asilimia 4 badala ya asilimia 6; Ada ya ukaguzi ni asilimia 0 badala ya
asilimia 1; na Kodi ya Ongezeko la Thamani asilimia 0, hivyo muuzaji wa dhahabu
anaweza kudai "input tax,” amesema Mhe. Mavunde.
Waziri Mavunde amemalizia kwa kusema
kuwa chini ya mpango huu, wamiliki wa leseni ya uchimbaji wa madini,
wafanyabiashara wakubwa wa madini na viwanda vya kuchenjulia dhahabu wanaweza
kuiuzia Benki Kuu kiasi chochote cha dhahabu.
0 Maoni