Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na
Uratibu) William Lukuvi amesema Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ameagiza
kurejeshwa huduma za kijamii, kuruhusu kufanyika kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa
na kuondolewa vikwazo vyote vilivyowekwa kwa wakazi wa Tarafa ya Ngorongoro.
Hatua hiyo inafuatia wakazi hao kukusanyika kwa siku tano mfululizo
katika maeneo tofauti wakidai kupatiwa haki hizo, zikiwamo za huduma za elimu,
afya na maji pamoja na kuondolewa vikwazo vya kuingia na kutoka eneo hilo la
Ngorongoro.
Wakazi hao ambao awali waliandamana kupinga kufutwa
vitongoji 96, vijiji 25 na kata 11, amri ambayo kimsingi ilikuwa ikiwakosesha haki
ya kupiga kura, na kuwanyima haki ya kuwachagua viongozi wao.
Waziri Lukuvi alitoa kauli hiyo leo akizungumza na wakazi hao wa kataa 11 leo katika eneo la Oloirobi lililopo Kata ya Ngorongoro, ambapo aliambatana na Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba Kabudi, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Danstan Kitandula, Mkuu wa Mkoa wa Arusha Paul Makonda na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi Awadh Juma Haji.
0 Maoni