Kamati ya Bunge yapongeza utekelezaji wa REGROW

 

Wizara ya Maliasili na Utalii imepongezwa kwa usimamizi mzuri wa Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) kwa kuwa Mradi huo ni muhimu kwa uchumi wa Tanzania.

Pongezi hizo zimetolewa leo Agosti 13, 2024 na Kamati ya  Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii Jijini Dodoma, kwenye kikao maalumu kati ya Kamati hiyo na  Uongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa lengo la Kamati kupokea na kujadili Taarifa za utekelezaji wa mradi wa REGROW pamoja na Kanuni za Kifuta Jasho/Machozi.

Akijumuisha maoni ya Waheshimiwa Wabunge wa kamati hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya  Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe. Timotheo Mnzava (Mb), licha ya kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayoifanya katika kukabiliana na changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa mradi, ameiagiza Wizara kuhakikisha inasimamia vyema Mradi huo ili ukamilike kwa wakati uliopangwa.

Mhe. Mnzava ameongeza kuwa, Mradi huo ni muhimu kwa maendeleo ya Sekta ya Maliasili na Utalii, nchi pamoja na uchumi wa nchi hivyo usimamizi madhubuti unahitajika ili ukamilike mapema kama ilivyopangwa ili watanzania waweze kufaidi matunda ya uwepo wa mradi huo.

Aidha, Mhe. Mnzava amesisitiza kuwa, Wizara iendelee kuchukua tahadhari kubwa kwenye utekelezaji wa mradi ili kuepusha vikwazo vyovyote katika utekelezaji wa mradi kwa wakati.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) ameishukuru kamati hiyo kwa kuendelea kushirikiana na kuishauri Wizara katika kutekeleza majukumu yake hali ambayo inachochea ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu ya Wizara.

Mhe. Kairuki ameihakikishia Kamati hiyo kufanyia kazi maagizo yote yaliyotolewa na Kamati hususani la kuhakikisha kasi ya utekelezaji wa mradi wa REGROW inaongezeka ili ujenzi unaoendelea ukamilike kwa wakati na pia ameialika kamati hiyo kufanya ziara kujionea hatua za utekelezaji wa mradi kwa sasa.

Aidha, kuhusiana na masuala ya kifuta jasho/machozi, Mhe. Kairuki amefafanua kuwa Serikali hususan Wizara ya Maliasili na Utalii inafedheheshwa na changamoto zinazosababishwa na wanyamapori wakali na waharibifu na kuahidi kuendelea kufanyia kazi changamoto hizo na kupokea ushauri wa kamati.

Pia amesema katika kukabiliana na changamoto hizo, Wizara inaendelea kugawa mabomu ya kufukuza tembo katika Wilaya mbalimbali nchini zinazokabiliwa na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu na imeweza kuanzisha Mfumo wa kielektroniki wa ukusanyaji na uwasilishaji wa taarifa za matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu [Problem Animals information System-PAIS].

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii imekutana na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kupata taarifa za utekelezaji wa mradi wa REGROW na kupitishwa kwenye  Kanuni ya Kifutajasho na Kifutamachozi ya mwaka 2011 pamoja na marekebisho yake.

Chapisha Maoni

0 Maoni