Wazee wa kata ya Kanyelele wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza
wamemsimika Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi wa Polisi DCP
Wilbrod Mutafungwa kuwa Mtemi wao na kumpa jina la Sangija
Wazee hao wamesema wamefikia uamuzi huo kutokana kuridhishwa
na utendaji kazi wa kamanda huyo pamoja na watendaji wengine wa jeshi la polisi
katika Mkoa wa Mwanza.
Thomas Shunashu ni Mtendaji wa kata ya Kanyelele amesema
kata hiyo yenye wakazi zaidi ya elfu kumi na tano ina vijiji vitano ambapo
wakazi wake wameelimika na kuacha kuwapiga wahalifu pindi wanapowakamata.
"Katika kata hii ya Kanyelele wakazi wote
wameshaelimishwa na polisi kata hakuna mtu anayempiga mhalifu wakimkamata
wanamkabidhi kwa jeshi la polisi na haya ni matokeo ya elimu ambayo polisi kata
amekuwa akiitoa mara kwa mara, sasa hivi Kanyelele ipo shwari kabisa sungusungu
wapo macho muda wote na wanashirikiana vizuri na askari waliopo hapa.”
Kwa upande wake Diwani wa Kata hiyo ya Kanyelele Daniel
Makoye akampongeza Kamanda Mutafungwa kufika katika kijiji cha Kanyelele na
kuzungumza na wakazi wake ambao kutokana na utendaji wake wa kazi wakaamua
kumsimika kuwa Mtemi wao na kumpa jina la Sangija.
"Kwakweli kamanda Mutafungwa umekuwa kamanda wa mfano
katika mkoa huu kwa kuweza kuwafikia wananchi walipo hata mimi leo siamini kama
umeweza kufika Kanyelele nikupongeze sana kwa kazi nzuri unayoifanya na
wananchi hawa kuamua kukusimika kuwa mtemi wao ni kutokana na utendaji wako wa
kazi unaamua kutoka ofisini na kuwatembelea kujua changamoto zao kwa hilo
nikupongeze."
Jeshi la polisi mkoa wa Mwanza limekuwa likifanya mikutano ya mara kwa mara na wakazi wake kwa lengo la kufahamu changamoto wanazokutana nazo na kuzitafutia ufumbuzi kwa kuendelea kuimarisha ulinzi na usalama kwa wakazi hao.
Wazee wa Kata ya Kanyelele wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza wakimsimika Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi wa Polisi DCP Wilbrod Mutafungwa kuwa Mtemi wao na kumpa jina la Sangija.
Wakazi wa Kata ya Kanyelele wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza wakifuatilia hafla ya kusimikwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi wa Polisi DCP Wilbrod Mutafungwa kuwa Mtemi wao na kumpa jina la Sangija.
0 Maoni