ADHA YA TEMBO: Tembo 45 warejeshwa hifadhini

 

Serikali kupitia wizara ya Maliasili na utalii imezitaka Taasisi zilizopo chini ya Wizara hiyo kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero katika kutatua changamoto ya tembo ambao wanasababisha madhara kwa wananchi.

Akizungumza jana mbele ya mamia ya Wakazi wa Vijiji vya Mangae, Doma na Mkata Wilayani Mvomero, wakati wa Operesheni ya kuyarudisha makundi ya Tembo  Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Dunstan Kitandula (Mb),amesema kwa kutumia helikopta  makundi yenye jumla ya Tembo  45  waliokuwa kwenye maeneo ya  makazi ya wananchi yamerejeshwa hifadhini katika zoezi linaloendelea  kwa siku ya kesho.

Mhe, Kitandula ameeleza  zoezi la kuwarejesha  tembo hifadhini ni jitihada za makusudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu  ya Sita inayoongozwa na Mhe.Rais Dkt Samia Suluhu Hassan  katika kuwahakikishia usalama wananchi na uhifadhi endelevu  nchini.

"Zoezi hili la kutumia Helikopta limetumia gharama kubwa, lakini licha ya ukubwa wa gharama hizi Serikali imejipanga kupunguza kero kwa wananchi wa maeneo haya ambao kadhia za wanyama hawa zimekuwa zikihatarisha usalama na mali zao," alisema Mhe.Kitandula.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Bi, Judith Nguli akimuwakilisha mkuu wa Mkoa wa Morogoro, ameipongeza  Serikali  kupitia Wizara ya Maliasi na Utalii kuwezesha zoezi la kuwaswaga Tembo kwa kutumia Helikopta kwani changamoto  ya Tembo ni ya muda mrefu kwa wananchi.

kwa upande wake  Mbunge wa Mvomero, Mhe.Said Hussein Said amesema uwezeshaji wa zoezi  hilo ni faraja  kwa wananchi  kwani  tembo wamekua wakileta uharibifu  mkubwa wa mali na kuatarisha usalama wa Wananchi ambapo ameiomba Serikali  kuendelea kuwasaidia  kuepukana  na changamoto  hiyo.

"Naishukuru Serikali kusikia kilio cha wananchi na kuchukua hatua baada ya kuleta mapendekezo bungeni na kwa Waziri wa Maliasili na Utalii."

Akielezea vifaa vya kujikinga na tembo vilivyokabidhiwa na Wizara kwa wananchi, Mkurugenzi wa Taasisi ya Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) Dkt, Eblate Ernest Mjingo amesema Taasisi hiyo imeendelea kubuni mbinu mbadala za kutatua changamoto za migongano za kati ya binadamu na Wanyamapori nchini hususani tembo.

"Tafiti zimesaidia matumizi ya teknolojia katika kutatua migongano hiyo ikiwa ni pamoja na teknojia ya helkopta na mikanda ya visukuma mawimbi (GPS Coller)."

Uzinduzi rasmi wa Operesheni  hiyo  umefanyika katika Kijiji cha Maenga Wilaya ya Mvomero  na kuwajumuisha Viongozi wa Chama na Serikali na Viongozi wa kijamii wa Wilaya hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni