Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeendesha mafunzo
ya Usalama wa Anga kwa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa lengo
la kudhibiti vihatarishi mbalimbali vinavyoweza kujitokeza katika viwanja vya
ndege vinavyopatikana ndani ya shirika hilo, mafunzo yatakayochukua siku 5
kuanzia Machi 04, 2024 hadi Machi 08, 2024.
Akitoa mafunzo hayo Mkufunzi Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga
Tanzania (CATC) Thamarat Abeid alisema, "Lengo la mafunzo hayo ni kutoa
elimu inayohusiana na usalama wa viwanja
vya ndege ili kujua sheria, kanuni na taratibu za Shirika mama la Usafiri wa
Anga duniani - ICAO pamoja na kanuni na taratibu ambazo zimetolewa na Mamlaka
ya Usafiri wa Anga Tanzania - TCAA ili wataalam wetu hawa wafanye kazi kwa
ufasaha na kuleta tija kwa taifa na dunia kwa ujumla".
Aidha, mkufunzi huyo aliongeza kuwa mafunzo haya yatahusisha
vihatarishi mbalimbali vilivyopo katika viwanja vya ndege, utoaji wa taarifa
ambazo ni muhimu sana ili wamiliki wa ndege na marubani wapate wigo mpana wa
uelewa hata kama itatokea changamoto ijadiliwe kwa pamoja na kupata muafaka wa
pamoja kati ya wamiliki wa viwanja, marubani, wamiliki wa ndege na Mamlaka ya
Usafiri wa Anga.
Naye, Afisa Uhifadhi Mkuu anayesimamia viwanja vya ndege
TANAPA Christine Bgoya alisema, kwenye mafunzo haya tunao Maafisa na Askari
kutoka Idara za Utalii na Miundombinu ambao wanahusika moja kwa moja na masuala
haya ya viwanja vyetu vya ndege, hivyo kuwepo kwao hapa kutawaongezea uelewa wa
kuviendesha viwanja hivi kitaalam zaidi tofauti na ilivyokuwa awali.
Pia, Mhifadhi Bgoya aliongeza, "Lengo la kuomba mafunzo
haya kutoka kwa wenzetu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga ni kutokana na ongezeko
kubwa la idadi ya watalii wanaotumia usafiri wa anga, mathalan kwa takwimu za mwaka huu kwa Hifadhi ya Taifa
Mikumi zaidi ya nusu ya watalii wote wa
nje hutumia ndege, hivyo ni wakati muafaka kwa TANAPA kupata mafunzo
haya."
Vilevile, Kamishna Msaidizi Fredrick Malisa akimwakilisha
Kamanda Uhifadhi Kanda ya Mashariki, aliwashukuru wakufunzi hao kwa mafunzo
hayo na kuwadokeza kuwa usafiri wa anga kwa upande wa TANAPA ni nguzo muhimu
sana katika mnyororo wa kukuza utalii nchini.
Aidha, Kamishna Malisa alisema, "Shirika linatambua
kwamba ili kazi za usalama wa viwanja vya ndege zifanyike kwa ufanisi ni lazima
watumishi wanaofanya kazi hizo kujengewa uwezo, na ndio maana leo tuko hapa
tukipewa mafunzo ya kibobezi na wataalam wetu kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Anga
Tanzania. Hivyo tuwahakikishie hayo yote mnayotufundisha tutayafanyia
kazi."
Mafunzo hayo ya usalama wa viwanja vya ndege yanafanyika kwa
siku tano mfululizo kuanzia leo Machi 04, hadi 08, 2024 katika Hifadhi ya Taifa
Mikumi iliyoko mkoani Morogoro.
Na. Zainab Ally- Mikumi
0 Maoni