Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kuinua uchumi- Jafo

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesema Mradi wa EBARR ambao unasimamiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais umekuwa na lengo la kuinua uchumi kwa wananchi kujipatia kipato nje ya shughuli zao za kila siku ambazo wanafanya.

Ameyasema hayo akikabidhi cherehani 21 kwa vikundi vitatu ikiwa sehemu ya wanufaika wa Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR) inayotekelezwa Wilayani Mpwapwa.

Pamoja na ugawaji wa cherehani hizo pia Waziri Dkt. Jafo alizindua Mradi wa vikundi vitatu vya Ushonaji Kijiji cha Kiegea, Mbugani na Kijiji cha Kazania ikiwa pamoja na uzinduzi wa Kisima ambacho kinasaidia vijiji hivyo kupata maji kwa urahisi.

“Rais wa Jamhuri ya Mkuungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan alikusudia mradi huu utekelezwe hapa kwa lengo la kuhakikisha unasaidia na kubadilisha maisha ya watu wa eneo hili na umegharimu zaidi ya Shilingi bilioni 1.6 ili kutekeleza shughuli mbalimbali.

“Lengo la Rais, Samia ni kuona miradi hii inaendelea na kunufaisha watu, hivyo muhakikisha miradi hii inasimamiwa vizuri kwa kuwa unagusa eneo kubwa la maisha ya watu,” alisema Waziri Dkt. Jafo.

Diwani wa Kata ya Ngh’ambi, Richard Matonya alisema awali kabla ya mradi huo wananchi walikuwa wanakwenda kuchota maji umbali wa zaidi ya kilometa 10 lakini kwa sasa imesaidia hata kazi za kilimo ambazo wanakijiji hao wamekuwa wakifanya.

Mratibu wa EBARR kitaifa, Dkt. Makuru Nyarobi alisema lengo la miradi hii ni kuwasaidia wananchi katika shuguhuli zao hasa katika uchumi ndio maana imejikita zaida katika utekelezaji wake vijijini.

"Kuna wale wakulima walikuwa wanakwenda mbali kutafuta maji lakini sahivi imekuwa tofauti, wakulima nao wamefurahia lakini mafundi cherehani ambao wengi wao ni wakulima wanajipatia kipato kupitia ushonaji,” alisema Dkt. Nyarobi.

Mradi wa EBARR unatarajiwa kunufaisha zaidi ya kaya 29,000 na unakadiriwa kuwafikia wanufaika zaidi ya milioni moja (1,000,000) kupitia utekelezaji wa shughuli za miradi mbalimbali kama vile upatikanaji wa maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, kilimo na ufugaji, shughuli mbadala za kujiongezea kipato; na urejeshaji wa vyanzo vya maji.

Chapisha Maoni

0 Maoni