Mhe. Matiko akabidhiwa kero za Nyandoto Sekondari

 

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mara Mhe. Esther Nicholas Matiko amefika Shule ya Sekondari Nyandoto iliyopo Halmashauri ya Mji wa Tarime na kuzungumza na Walimu na Wanafunzi wa Shule hiyo.

Akizungumza na Walimu wa Shule hiyo, Mhe. Esther Matiko amepokea changamoto zinazoikabili Shule hiyo ikiwa ni pamoja na ukosefu wa huduma ya Maji shuleni hapo, ukosefu wa Mabweni kwa Wanafunzi, upungufu wa vifaa vya kufundishia (Vitabu vya Masomo ya Sanaa), miundombinu mibovu ya barabara kufika shuleni hapo nk.

Mhe. Esther Matiko ametumia nafasi hiyo kuwapongeza Walimu wa Shule hiyo kwa kuendelea kufanya kazi kwa Moyo mmoja na bidii licha ya changamoto kadhaa kuwepo zinazoikabili Shule hiyo. Sambamba na hilo Mhe. Matiko ameahidi kwenda kuzisema changamoto hizo Bunge la Bajeti linalotarajiwa kuanza mwezi wa nne Jijini Dodoma.

Akizungumza na Wanafunzi wa Nyandoto Sekondari, Mhe. Matiko amewahasa Wanafunzi wa Shule hiyo kutumia muda wao vizuri kwa kujisomea na kuachana na tabia ya kwenda kujishughulisha na shughuli za Machimbo (Mgodi) yanayopatikana eneo la Kewamamba Jimbo la Tarime Vijijini.

Mhe. Esther Matiko amewahimiza pia Wanafunzi hao kujishughulisha na michezo kwa kuwapatia Mpira wa Miguu na Mpira wa Pete kwani michezo imekuwa yenye manufaa makubwa hivi sasa kwa kutoa ajira, kuimarisha afya na kujenga mahusiano.

Akizungumza kwa niaba ya Walimu, Mkuu wa Shule hiyo Mwl John Magesa amemshukuru na kumpongeza Mhe. Esther Matiko kwa namna anavyojitoa kuhakikisha watoto wa Tarime wanafanikiwa kufikia malengo yao kupitia elimu kwa kuwapa hamasa, husia na kutoa vifaa mbalimbali vya kielimu mashuleni.

Peter Magwi Michael- Mara

Chapisha Maoni

0 Maoni