Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na
Leseni (BRELA), Bw. Godfrey Nyaisa leo tarehe 7 Machi, 2024 amekutana na
kufanya mazungumzo na Mwanamuziki wa kizazi kipya na Mkurugenzi wa Wasafi
Media, Bw. Naseeb Abdul maarufu kwa jina la Diamond Platnumz alipotembelea
katika Ofisi za BRELA jijini Dar es Salaam.
Bw. Abdul amesema mbali na kuwa mwanamuziki yeye ni
mfanyabiashara na mwekezaji ambaye hutengeneza na kuanzisha chapa na kuwainua
vijana ili kujipatia kipato hivyo kama mfanyabiashara BRELA ni kama nyumbani.
“Nilipokutana na Bw.Godfrey Nyaisa na kujitambulisha kwangu
alinieleza kuwa, BRELA panafaa kuwa
nyumbani kwako kwasababu una chapa tofauti tofauti hivyo patakusaidia
katika kusajili kazi zako ili usipoteze haki, maneno hayo yalikuwa na maana
kubwa katika maisha yangu na hapo ndipo nilipobadilisha mtazamo na kugundua
vijana wengi wanapoteza haki zao,” ameeleza Bw. Abdul.
Ameendelea kusema kuwa, wasanii, wanamichezo, vijana na yeyote
mwenye lengo la kufika mbali kimaendeleo hawezi kwenda mbele kama hajarasimisha
biashara yake BRELA na ili kuwa rasmi unahitaji kusajili jina la biashara,
kusajili kampuni na kufuata taratibu mbalimbali ambazo serikali wameweka kama
njia nzuri ambazo zitalinda na kuwezesha kufika mbali.
Aidha, amesisitiza kuwa ni vyema kujitahidi kujirasimisha na
kulinda alama ya biashara na huduma pamoja na vumbuzi BRELA ili kulinda ndoto
yako kwasababu ukianzisha jambo na likawa kubwa ukigundua kuna mtu anatumia
alama yako, kama yeye amewahi ameisajili kisheria anauwezo wa kukupeleka katika
vyombo vya sheria.
“Kwa watu ambao wanatumia brand zetu pasipo kuwa na haki
halali naelewa kibinadamu atakuwa anatafuta riziki lakini nawashauri waache na
wasinilaumu baadae kwasababu sheria
itafuata mkondo wake hasa kwa kipindi hiki tumeamua kuwa makini zaidi katika
biashara,” ameendelea kusisitiza Bw Abdul.
Amehitimisha kwa kusema kuwa sasa amegundua umuhimu wa sajili
na amefanikiwa kuchukua hatua ya kulinda haki zake BRELA baada ya kufahamu kwa
kina faida zake hivyo kuepuka hasara kubwa ambayo angeipata na kupelekea
kupoteza pato la Taifa.
0 Maoni