Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Ashatu Kijaji amewataka
wajasiriamali wanawake wanaoendesha biashara zao sokoni kurasimisha biashara
zao na kuzisajili kwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA). Hii
itaziongezea thamani na kulinda bunifu zao na kuwawezesha kunufaika nazo
kiuchumi.
Mhe. Dkt. Kijaji ametoa rai hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa
niaba yake na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa, leo Machi 7,
2024 ikiwa ni maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyoandaliwa na
Wanawake wa Masokoni wa Mkoa wa Dar es Salaam (WOMEN TAPO) yaliyofanyika katika
Viwanja vya Mnazi Mmoja, Jijini Dar es Salaam.
Katika hafla hiyo, Bw. Nyaisa amewataka wanawake
wajasiriamali kuacha kuendesha biashara
kienyeji na kuwaeleza faida watakazopata kwa kusajili biashara na
vumbuzi zao itakayowawezesha kupata fursa mbalimbali za kibiashara na ulinzi wa
kisheria.
“Niwahakikishie kuwa BRELA inazipa ulinzi wa kisheria
biashara na bunifu iwapo mtu yeyote ataiga kazi yako, kwa wewe mwanamke
mjasiriamali uliye na usajili wa BRELA una haki ya kushtaki mahakamani na
Wakala itasimama kukutetea kuwa hiyo ni mali yako” ameeleza Bw. Nyaisa.
Amewasisitizia kuongeza thamani bidhaa zao wanazozalisha kwa
kuweka alama ya biashara kwenye bidhaa zao wanazozizalisha ili kutambulika kwa
uharaka katika masoko na kuweza kuzitofautisha na bidhaa zingine.
Ameongeza kuwa mbali ya kupata ulinzi wa kisheria pia
watapata fursa ya kukopesheka katika Taasisi rasmi za Kifedha ambako moja ya
masharti lazima uwe umesajili biashara yako BRELA badala ya kuchukua mikopo
umiza.
0 Maoni