Wanawake Wajasiriamali zipeni ulinzi alama za biashara zenu

 

Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Ashatu Kijaji amewataka wajasiriamali wanawake wanaoendesha biashara zao sokoni kurasimisha biashara zao na kuzisajili kwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA). Hii itaziongezea thamani na kulinda bunifu zao na kuwawezesha kunufaika nazo kiuchumi.

Mhe. Dkt. Kijaji ametoa rai hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa, leo Machi 7, 2024 ikiwa ni maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyoandaliwa na Wanawake wa Masokoni wa Mkoa wa Dar es Salaam (WOMEN TAPO) yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, Jijini Dar es Salaam.

Katika hafla hiyo, Bw. Nyaisa amewataka wanawake wajasiriamali kuacha kuendesha biashara  kienyeji na kuwaeleza faida watakazopata kwa kusajili biashara na vumbuzi zao itakayowawezesha kupata fursa mbalimbali za kibiashara na ulinzi wa kisheria.

“Niwahakikishie kuwa BRELA inazipa ulinzi wa kisheria biashara na bunifu iwapo mtu yeyote ataiga kazi yako, kwa wewe mwanamke mjasiriamali uliye na usajili wa BRELA una haki ya kushtaki mahakamani na Wakala itasimama kukutetea kuwa hiyo ni mali yako” ameeleza Bw. Nyaisa.

Amewasisitizia kuongeza thamani bidhaa zao wanazozalisha kwa kuweka alama ya biashara kwenye bidhaa zao wanazozizalisha ili kutambulika kwa uharaka katika masoko na kuweza kuzitofautisha na bidhaa zingine.

Ameongeza kuwa mbali ya kupata ulinzi wa kisheria pia watapata fursa ya kukopesheka katika Taasisi rasmi za Kifedha ambako moja ya masharti lazima uwe umesajili biashara yako BRELA badala ya kuchukua mikopo umiza.

Chapisha Maoni

0 Maoni