Kamati yatumia ndege kukagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua Ihefu

 

Kamati ya Maafa wilayani Mbarali ambayo Mwenyekiti wake ni Mkuu wa Wilaya ya Mbarali Mhe. Denis Mwila kwa kushirikiana na Diwani wa Kata ya Luhanga Mhe. Baraka Mamboleo, wametembelea na kukagua maeneo ya Kata ya Luhanga yaliyoathiriwa na mafuriko ya mvua zilizonyesha kati ya tarehe 30/01/2024 hadi tarehe 03/02/2024 na kusababisha wananchi kuyakimbia makazi yao kutokana na kuzingirwa na maji.

Ili kuwafikia wahanga hao kwa haraka zaidi, Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA Musa Nassoro Kuji alitoa ndege ya kuzungukia maeneo yote yaliyoathirika ili kamati ya maafa wilaya ya Mbarali ifanye tathmini ya ukubwa wa tatizo. Aidha Kamishna huyo pia, aliwaagiza maafisa na askari wake kutoka Kanda ya Kusini na Hifadhi ya Taifa Ruaha kushirikiana na Kamati hiyo pamoja na uongozi wa kijiji ili kunusuru hali hiyo.

Akitoa maelezo ya mafuriko hayo, Diwani wa Kata ya Luhanga Mhe. Mamboleo aliyekuwa ndani ya ndege hiyo huku akionyesha baadhi ya maeneo yaliyoathirika alisema, "Tathimini iliyofanywa na viongozi wa kijiji na vitongoji, wamebaini kuwa, vitongoji vya Matono na Iyala vimeathiri zaidi na mafuriko. Jumla ya nyumba kumi na saba (17) zimesombwa na maji na kusababisha familia kadhaa kukosa makazi, na familia nyingine zimejiegesha kwa muda katika shule ya Msingi Iyala huku taratibu nyingine za kiserikali zikiendelea kufanyika."

Naye, Mwakilishi wa Mratibu wa Maafa Wilaya ya Mbarali, ambaye ni Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo- Ndg. Ray Salandi alisema, "Kutokana na makazi mengi kuzingirwa na maji, mazingira hayo sio rafiki kabisa kwa maisha ya binadamu hususan ikitokea mlipuko wa magonjwa ya kuhara au kipindupindu wananchi wengi wataathirika zaidi, hivyo nawasihi wananchi hawa waondoke haraka  kuelekea maeneo salama wakati huu ambapo kivuko cha daraja kilichokuwa kimezama kutokana na wingi wa maji kimeanza kupitika baada ya maji kupungua.

Kamati ya maafa imewataka wananchi wanaoishi maeneo yaliyokumbwa na mafuriko kuondoka mara moja ili kupunguza maafa yanayoweza kutokea wakati huu na baadae. Kwani tunakoelekea ni msimu wa mvua nyingi za masika.

Zoezi la kuyazungukia maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko lililofanyika jana tarehe 07.02.2024 lilisimamiwa na kuratibiwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbarali akishirikiana na TANAPA.

Na.Jacob Kasiri - Mbarali

Chapisha Maoni

0 Maoni