Ujenzi wa daraja la Bibi Titi kugharimu shilingi bilioni 11

 

Mradi wa Ujenzi wa daraja la Bibi Titi Mohamed uliopo Kata ya Mohoro , Rufiji utakaogharimu shilingi bilioni 11 umekabidhiwa rasmi leo tarehe 26 Januari, 2024 kwa Mkandarasi  Mzawa MAC Contractor.

Makabidhiano hayo yaliyofanyika katika ofisi ya Serikali ya kijiji cha Shela yameshuhudiwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff pamoja na Viongozi wa Serikali ya Kijiji na Wananchi.

Katika kikao hicho Mhandisi Seff amemtaka Mkandarasi huyo kufanya kazi na timu ya watendaji wote wa mradi kwa mujibu wa mkataba ili kazi zitekelezwe kwa ufanisi na kukamilika kwa wakati.

Naye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Rufiji na Diwani wa Kata ya Mohoro Mhe. Abdulrahman Chobo amemshukuru Mtendaji Mkuu wa TARURA  kwa ushiriki wake kwenye kikao hicho na kuahidi kwamba wananchi wa Kata ya Mohoro watatoa ushirikiano mkubwa kwa Mkandarasi huyo wakati wa ujenzi ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Mkataba wa ujenzi wa daraja hilo ulisainiwa tarehe 1 Disemba,2023 na jiwe la msingi liliwekwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa.



Chapisha Maoni

0 Maoni