Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Amos Makalla amewaagiza wataalam wa
afya wa wilaya zote katika mkoa huo kuweka mikakati ya kudhibiti na kuhudumia
wagonjwa wa kipindupindu kufuatia kuwepo kwa wagonjwa 28 wa ugonjwa wa
kipindupindu mkoani humo.
Makalla ametoa wito huo leo Januari 10, 2024 wakati wa kikao
chake na wajumbe wa Kamati ya Huduma ya Afya ya Msingi mkoani humo ili
kuwekeana mikakati ya kudhibiti kusambaa kwa ugonjwa huo ulioanzia Wilayani
Magu.
"Tuelewane wataalam wa afya, kama leo tuna wagonjwa 28,
tukitoka hapa nataka tudhibiti ugonjwa huu usienee mkoani hapa na ili
kufanikisha hilo ni lazima tuwe na mikakati ya pamoja ya makusudi ya kudhibiti
tatizo hili lisisambae tena kwa ushirikiano mkubwa," amesema Makalla.
Aidha, Makalla amebainisha kuwa kipindupindu kinatokana na
vimelea vya uchafu vitokanavyo na matendo kama chakula kuandaliwa bila kunawa
mikono na kupelekea mtu kula uchafu na kama mtaani watu wataendelea kuwa na
utamaduni wa mama ntilie kuuza chakula kwenye mazingira yasiyo masafi na kwamba
mazingira hayo yatafanya ugonjwa kuendelea kusambaa.
"Nataka miwaambie wananchi kwamba hakuna gharama zozote
kwa mgonjwa wa kipindupindu kutibiwa, mtu yeyote mwenye dalili za Ugonjwa wa
Kipindupindu afikishwe hospitalini haraka na sio kumhudumia nyumbani au kwa
waganga wa kienyeji na serikali tumejipanga kuwahudumia," amesisitiza
Makalla.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Dr Thomas Rutachunzibwa
amebainisha kuwa hadi sasa wilaya zilizoathirika ni tatu za Magu, Nyamagana na
Ilemela huku Magu ikiathirika zaidi kwa kuwa na wagonjwa 21 hadi sasa na kwamba tayari kuna vituo vitatu
vya kutolea huduma kwa wagonjwa wa kipindupindu.
"Dalili za kipindupindu zinaanza kujitokeza ndani ya masaa 24 hadi 72 baada ya kupata maambukizi na mtu hukosa maji mwilini kutokana na kutapika na kuharisha hivyo jamii lazima iwe na matumizi sahihi ya vyoo, kuosha chakula kama matunda kwa maji ya moto, kutumia maji yaliyochemshwa na kuchunjwa vizuri," ameeleza Dkt. Rutachunzibwa.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Huduma ya Afya ya Msingi wa mkoa wa Mwanza wakisikiliza kwa makini maagizo ya Mkuu wa Mkoa Makalla kuhusiana na mikakati ya kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu mkoani huo.
0 Maoni