Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema kazi inayofanywa na taasisi za elimu ya juu
ni kielelezo cha mchango wa sekta
binafsi kuchangia maendeleo ya Zanzibar
kwa kuandaa wataalamu wa fani mbalimbali.
Rais Dk.Mwinyi amesema hayo katika Mahafali ya 23 ya Chuo
Kikuu cha Abdulrahman Al -Sumait Chukwani, Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe: 27
Januari 2024.
Aidha Rais Dk.Mwinyi amepongeza juhudi zinazofanywa na Chuo
hicho kinachomilikiwa na Shirika la Direct Aid ya Kuwait kwa mchango wake
katika maendeleo ya sekta ya elimu Zanzibar tangu kuanzishwa kwake 1998.
Rais Dk. Mwinyi
amevihimiza vyuo kujikita katika utafiti utakaotoa ufumbuzi wa changamoto
zinazoikabili jamii kwa kushirikiana na taasisi na idara mbalimbali za
Serikali.
Kwa upande mwingine Rais Dk.Mwinyi amevitaka vyuo kikuu
kuongeza programu zinazoakisi mahitaji ya nchi ikiwemo zinazohusu uchumi wa
buluu.
Mahafali hayo yamehudhuriwa na Mkuu wa Chuo cha Abdulrahman Al-Sait, Rais Mstaafu Mhe.Dkt Amani Abeid Karume, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mhe. Lela Mohamed Mussa , Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe.Idrissa Kitwana Mustafa pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, wa Dini na Vyombo vya ulinzi na usalama.
0 Maoni