Korea yatoa msaada wa magari ya kisasa ya kubebea wagonjwa Mloganzila

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila imepokea msaada wa magari mawili ya kukubea wa wagonjwa (ambulances) kutoka Serikali ya Korea Kusini kupitia Taasisi yake ya Korea Foundation for International Health Care (KOFIH) wenye thamani ya takribani TZS. Mil 372.

Akipokea magari hayo kwa niaba ya Waziri wa Afya, Mkuu wa Idara ya Matibabu nje ya nchi, Wizara ya Afya Dkt. Asha Mahita ameishukuru Serikali ya Korea Kusini kwa ushirikiano unaoendelea kutoa katika kuboresha huduma za afya hapa nchini.

“Kwa niaba ya Serikali ninawashukuru sana kwa msaada huu kwani mmeunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo hivi karibuni ilinunua na kusambaza magari ya kubebea wagonjwa zaidi ya 600. Magari hayo yalisambazwa nchi nzima ikiwa ni jitihada za kuhakikisha kuwa hakuna Mtanzania anayepoteza maisha anapopata ajali au ujauzito,” Dkt. Asha.

Dkt. Asha ameongeza kuwa lengo la Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha kuwa Tanzania inakuwa kitovu cha tiba utalii Afrika Mashari na Kusini mwa Jangwa la Saraha kwa kutoa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi zenye ubora wa hali juu katika ukanda huo.

Kwa upande wake, Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Dkt. Kim Sun Pyo ameupongeza uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili -Mloganzila kwa kuendelea kuimarisha huduma ambazo zimeifanya kuwa tegemeo nchini.

Dkt. Pyo ameongeza kuwa Serikali yake kupitia KOFIH imetoa msaada huu kwa kutambua kuwa uhai wa watu ni muhimu sana na kubainisha kuwa magari ya kubebea wagonjwa yana nafasi kubwa katika kuokoa maisha ya mwanadamu.

Naye, Naibu Mkurugenzi Mtendaji MNH-Mloganzila Dkt. Julieth Magandi amesema magari hayo yametengenezwa mwezi Agosti 2023 hivyo ni ya kisasa na yana vifaa tiba ambayo ni nadra sana kuvipata katika magari mengine ya kubebea wagonjwa.

Akitoa shukurani kwa niaba ya wafanyakazi wa MNH -Mloganzila, Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Tiba, Dkt. Faraja Chiwanga amesema magari hayo yamesaidia kutatua changamoto za magari ya kubebea wagonjwa hospitalini hapa ambayo yalikuwa machache na mengine chakavu.

Chapisha Maoni

0 Maoni