Kamati ya Bunge yakoshwa mkakati kutokomeza ukatili

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Ustawi na Maendeleo ya Jamii imeridhishwa na utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto MTAKUWWA wa mwaka 2017/18-2021/22.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Riziki Lulida akizungumza wakati wa kikao cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa Mpango huo kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, jijini Dodoma Januari 22, 2024 amesema

Wizara hiyo inafanya kazi kubwa hivyo ni jukumu la Kamati kuhakikisha bajeti ya utekelezaji wa majukumu yake inaongezwa.

Mhe. Riziki ameitaka Wizara kuangalia zaidi wanawake na watoto wenye ulemavu sambamba na suala zima la mmomonyoko wa maadili unaochochewa na baadhi ya vipindi kwenye baadhi ya Vyombo vya Habari nchini.

Miongoni  mwa wajumbe wa Kamati hiyo Mhe. Neema Lugangira akichangia mjadala wa taarifa hiyo, ametoa pongezi kwa Wizara kwa kazi kubwa ya MTAKUWWA iliyowezesha kuongezeka kwa wananchi kutoa taarifa kutokana na kuwa na imani na Serikali kufanyia kazi.

Mhe. Neema amempongeza pia Waziri Dkt. Dorothy Gwajima kwa jitihada zake binafsi za kujibu haraka hoja za wananchi hasa upande wa mitandao ya kijamii na kuzifanyia kazi kwa wakati kisha kuishauri Wizara kushughulikia ukatili wa kijinsia kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu hasa kwa wanafunzi wenye mahitaji Maalum.

Rugangira ameiomba Wizara kuangalia pia ukatili wa wanawake na watoto kwenye  mitandao ya kijamii, wanawake wafanyabiashara na wanasiasa kwani wanapitia zaidi ukatili wa kijinsia.

Naye Mhe. Katani Katani ameishauri Wizara kuandika andiko mahususi la kuomba fedha kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yake hasa yale ya kipaumbele, ili kuwezesha Kamati hiyo kujenga hoja ya kuongezwa kwa Bajeti.

Kwa upande wake Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima ameishukuru Kamati hiyo kwa kuelewa ukubwa wa Wizara na majukumu yake kwa mustakabali wa Taifa na kuwaomba wajumbe wa Kamati hiyo kuendelea kushauri wadau wengine ili mapinduzi ya uendeshaji yafanyike kama timu moja na kuleta uwajibikaji wa pamoja.

Amesema Kamati hiyo ina ukubwa wa kuweza kuunganisha Kamati nyingine zote pamoja na Wizara za Kisekta katika kuwekeza kwenye Ajenda ya Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto kwani ndio waathirika wakubwa ukatili.

Akiongea wakati wa kikao hicho Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Seif Shekalaghe ameihakikishia Kamati hiyo kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na kuyafanyia kazi ili mpango mpya wa kutokomeza ukatili ufanyike kwa ufanisi.

Na. WMJJWM- Dodoma

Chapisha Maoni

0 Maoni