Waliokufa kwenye maporomoko ya matope Hanang wafikia 80

 

Idadi ya watu waliokufa kwenye maporomoko ya matope ya Mlima Hanang yaliyotokea wilayani Hanang mkoani Manyara yaliosababishwa na mvua imeongezeka na kufikia watu 80, huku mwili mmoja wa mwanamke ukipatikana hii leo.

Akiongea na waandishi wa habari leo huko Katesh Msemaji Mkuu wa Serikali Bw. Mobhare Matinyi ametoa mchanganuo wa waliokufa kuwa watu wazima ni 48 (wanaume 19 na wanawake 29) na watoto ni 32 (wa kiume 15 na wa kike 17).

Matinyi amesema mwili mmoja wa mtoto wa kiume ambao ulikuwa haujatambuliwa hadi jana sasa umetambuliwa lakini kuna mwili wa mwanamke mmoja mtu mzima uliopatikana leo ambao bado haujatambuliwa. Hivyo, jumla ya maiti zilizokwishatambuliwa hadi sasa ni 79.

Maafa ya maporomoko ya matope yaliziathiri kata za mji mdogo wa Katesh za Jorodom, Ganana, Katesh na Dumbeta pamoja na vijiji vya Sarijandu, Arukushay na Sebasi vya kata ya Gendabi, vyote kwenye tarafa ya Katesh, wilayani Hanang, mkoani Manyara.

Chapisha Maoni

0 Maoni