NGOs zatakiwa kuhuisha taarifa zao kwenye mfumo wa kigitali (NIS)

 

Wataalam kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum wamewahimiza wadau wanaoendesha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali mkoani Mtwara kuhuisha taarifa sahihi na muhimu juu ya Mashirika yao katika mfumo wa kidigitali ulioboreshwa (NIS).

Hayo yameelezwa katika mkutano wa majumuisho baina ya Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Mkoa wa Mtwara Abdillah Mfinanga, Wataalam kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii na Wawakilishi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Desemba 21,2023.

Akizungumza katika kikao hicho Katibu Tawala Msaidizi Abdillah Mfinanga amefafanua kwamba ulipaji wa ada peke yake hautoshi kulitambulisha Shirika kuwa hai na kuna ulazima wa kila Shirika kujaza taarifa zinazotakiwa ili kurahisha ufuatiliaji wa Shirika na kazi wanazofanya.

“Tumekadiriwa kuwa na asilimia 50 katika zoezi zima la ujazaji wa taarifa na hiki si kitu kizuri, natumaini tutabadilika na kuhuisha taarifa zinazoendana na mfumo ulioboreshwa (NIS) ili kurahisisha uratibu wa Mashirika yenu kwa Serikali na utambulishwaji wa huduma zenu kwa wanufaika lakini pia ufatiliaji wa taarifa kutoka kwa wafadhili” amesema Mfinanga.

Aidha Mtaalam kutoka Ofisi ya Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Charles Mpaka ameyahimiza Mashirika hayo juu ya umuhimu wa ushirikiano baina yao ili kukua na kustawi.

“Mashirika makubwa yanaweza kuyasaidia Mashirika machanga kukua kwa kuyashika mkono katika vitu vingi ikiwemo kuwaelekeza namna mzuri za uandishi wa Miradi, kuwasaidia na vitendea kazi pamoja na hata ushauri wa namna ya kuendesha miradi yao bila kusahau kuwaelekeza fursa zilipo” amesema Mpaka.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la PAWASO ambae ni mjumbe wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NACONGO) Mkoa wa Mtwara Baltazal Komba ameishukuru Serikali kwa jitihada zake katika kuimarisha mfumo mzima wa utoaji wa huduma kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali tofauti na awali.

Vilevile Mratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Mkoa wa Mtwara Tabitha Kirangi amesema zoezi hilo la ukaguzi wa Mashirika hayo umemrahisishia kuelewa vizuri changamoto zinazokabili Mashirika hayo na kuahidi kutoa ushirikiano wa karibu zaidi katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizo.

Na WMJJWM- Mtwara

Chapisha Maoni

0 Maoni