Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema matumizi ya mfumo wa PIPIMS,
PEPMIS na HR Assessment katika Utumishi
wa Umma nchini itaimarisha Utumishi wa
Umma kwa kuwabana Watumishi wanaopenda
kukaa ofisini pasipo kufanya kazi.
Mhe. Kikwete ametoa kauli hiyo leo Jijini Arusha wakati
akizungumza kwa nyakati tofauti na Watumishi wa
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha,
Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha ( AICC) na Chuo cha Ufundi Arusha
ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kukagua mafunzo ya matumizi ya
Mfumo wa Kupima Utendaji Kazi wa Watumishi wa Umma na Taasisi (PEPMIS na
PIPMIS) na Mfumo Maalum wa Tathmini ya hali ya Rasilimaliwatu Serikalini (HR
Assessment).
Amesema Serikali imedhamiria kuimarisha Utumishi wa Umma kwa
kuhimiza uwajibikaji ili kuhakikisha
kama Taifa linakuwa na utumishi wa umma unaopimika kwa kumpima Mtumishi mmoja mmoja pamoja na Taasisi kwa ujumla.
Ameongeza kuwa mfumo wa PEPMIS umekuja kuwa mbadala wa OPRAS
ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anayelenga
kuimarisha mifumo ya uwajibikaji inayowezesha viongozi na watumishi wa umma
kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi wakati na mahali popote.
Katika hatua nyingine Mhe. Kikwete amewataka Maafisa
Utumishi na Maafisa Tawala kuacha kukaa ofisini badala yake waende maeneo ya
kazi ili kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi walio chini yao.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe.John Mongela
amesema zama hizi hazihitaji watu wenye misuli kutokana na kukua na teknolojia.
Hivyo, teknolojia imerahisisha utendaji kazi na sisi tuko tayari kuisimamia
utekelezaji wake.
Amesema ujio wa mafunzo hayo
yamekuja wakati muafaka ambapo
Maafisa Utumishi na Maafisa Tawala wataanza kubadilika na kuachana na utaratibu wa kizamani wa utendaji
kazi wao.
Hata hivyo ametumia fursa hiyo kuiomba Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora kuwanoa upya Maafisa Utumishi na Maafisa Utawala wa mikoa na Halmashauri kwani utendaji wao wa kazi sio wa kuridhisha ikizingatiwa wao ndo wenye jukumu la kuwasimamia watumishi wengine.
Na Lusungu Helela- Arusha
0 Maoni