Maporomoko ya ardhi yaua watu 49 wilayani Hanang’

 

Watu wapatao 49 wamekufa na wengine 80 kujeruhiwa wilayani Hanang’ mkoani Manyara kufuatia kutokea kwa maporomoko ya ardhi katika Mlima Hanang’ leo asubuhi, yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

Mkuu wa Wilaya ya Hanang’, Janeth Mayanja amesema miili ya watu hao 49 imehifadhiwa katika hospitali ya Tumaini, na ametoa pole kwa wananchi wa Hanang’ kwa tukio hilo na kuwataka waendelee kuchukua tahadhari.

Janeth ameeleza kwamba tangu jana zilikuwa zinanyesha mvua za kawaida wilayani Hanang’ lakini anadhani kwamba mvua hizo zimesababisha kutokea kwa maporomoko ya ardhi kutoka katika Mlima Hanang’.

“Mvua zimesababisha maporokoko ya ardhi kwenye Mlima Hanang’ ambao pia huwa na chemichemi, maji yaliporomoka kutoka mlima huo yakiwa yamebeba mawe na miti katika Mji wa Katesh na katika Kata ya Gendabi,” alisema Janeth.

Amesema hadi sasa maji yanaendelea kutiririka kutoka Mlima Hanang’ na maji hayo yananguvu yamebeba matope, miti na mawe ukichanganya na maji ya mvua ambayo mvua inaendelea kunyesha yameleta athari kubwa na miundombinu imeharibika.

Mkuu wa Wilaya huyo amesema kwamba shughuli za uokoaji zinaendelea na kuongeza kwamba watu walioathiriwa na maporomoko hayo watahifadhiwa kwa muda katika shule mbili za sekondari na moja ya msingi.

Chapisha Maoni

0 Maoni