Tanzania imetajwa kuwa nchi ya kwanza
barani Afrika kwa kuwa na Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na
Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center
Situation Room) katika Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura
nchini ambacho kimeifanya nchi kuwa kinara katika masuala ya menejimenti ya
maafa hususan katika kuzuia, kupunguza kujiandaa na kukabili maafa pindi
yanapotokea.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu
anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ametoa kauli
hiyo jana Oktoba 23, jijini Windhoek nchini Namibia wakati akiwasilisha mada katika Kikao cha Tisa cha Jukwaa la
Kanda la Afrika la Kupunguza Madhara ya Maafa na Mkutano wa Nane wa Ngazi ya
Viongozi kuhusu masuala ya kupunguza madhara ya maafa.
Akizungumzia umuhimu wa kituo hicho,
Dkt. Yonazi amesema kituo hicho
kimeendelea kutumika kufanya ufuatiliaji wa uwezekano wa kutokea kwa
majanga kwa kutumia mifumo ya kiteknolojia ya kijiografia kwa majanga
yanayotokana na hali ya hewa na haidrolojia kwa kutumia jukwaa la kielektroniki
la MyDEWETRA.
“Mfumo huu umerahisisha ufuatiliaji wa
mwenendo wa janga lililotabiriwa na kufanya uchambuzi wa kiwango cha madhara
kwa jamii, miundombinu na mazingira, kuandaa taarifa za tahadhari ya mapema ya
hatua za kuchukua ili kuzuia, kujiandaa na kukabili maafa, kuandaa taarifa ya
mwenendo wa tukio na kusambaza kwa wadau mbalimbali kwa ajili ya kusaidia
uratibu na utekelezaji wa shughuli za kukabili na kurejesha hali,” amesema Dkt.
Yonazi.
Dkt. Yonazi amesema kuwa uanzishwaji
wa kituo hicho cha ufuatiliaji wa majanga na tahadhari ya mapema umefanikiwa
kutokana na mradi ulioanzishwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupunguza
Madhara ya Maafa katika Kanda ya Afrika na kufadhiliwa na Serikali ya Nchi ya Italia
kupitia Shirika la Maendeleo la Italia (Italian Agency for Development
Cooperation) ambapo Taasisi ya CIMA Research Foundation ya Italia imesadia
kutoa utaalam wa utekelezaji wa shughuli zote.
Kufuatia umuhimu wa kituo hicho, Dkt.
Yonazi ametoa wito kwa nchi wanachama pamoja
na mataifa mengine kuja Tanzania kwa
lengo la kujifunza na kubadilishana
uzoefu kwa kuzingatia umuhimu wake.
Tanzania ni miongoni mwa nchi
zilizoshiriki katika kikao hicho cha siku nne ambacho kimefanikiwa
kuwakutanisha wadau zaidi ya elfu moja wa
maafa kwa nchi za Afrika wakiwemo
wataalamu kutoka katika ngazi za
kitaifa, Serikali za mitaa, Mashirika ya Umoja wa Kitaifa na Kimataifa, Asasi
za Kiraia, sekta binafsi, taasisi za elimu na utafiti na waandishi wa habari.
0 Maoni