Tanzania yang’ara Kimataifa kwa Kituo cha Ufuatiliaji Majanga

 

Tanzania imetajwa kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kwa kuwa na Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room) katika Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura nchini ambacho kimeifanya nchi kuwa kinara katika masuala ya menejimenti ya maafa hususan katika kuzuia, kupunguza kujiandaa na kukabili maafa pindi yanapotokea.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ametoa kauli hiyo jana Oktoba 23, jijini Windhoek nchini Namibia wakati akiwasilisha mada katika Kikao cha Tisa cha Jukwaa la Kanda la Afrika la Kupunguza Madhara ya Maafa na Mkutano wa Nane wa Ngazi ya Viongozi kuhusu masuala ya kupunguza madhara ya maafa.

Akizungumzia umuhimu wa kituo hicho, Dkt. Yonazi amesema kituo hicho  kimeendelea kutumika kufanya ufuatiliaji wa uwezekano wa kutokea kwa majanga kwa kutumia mifumo ya kiteknolojia ya kijiografia kwa majanga yanayotokana na hali ya hewa na haidrolojia kwa kutumia jukwaa la kielektroniki la MyDEWETRA.

“Mfumo huu umerahisisha ufuatiliaji wa mwenendo wa janga lililotabiriwa na kufanya uchambuzi wa kiwango cha madhara kwa jamii, miundombinu na mazingira, kuandaa taarifa za tahadhari ya mapema ya hatua za kuchukua ili kuzuia, kujiandaa na kukabili maafa, kuandaa taarifa ya mwenendo wa tukio na kusambaza kwa wadau mbalimbali kwa ajili ya kusaidia uratibu na utekelezaji wa shughuli za kukabili na kurejesha hali,” amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amesema kuwa uanzishwaji wa kituo hicho cha ufuatiliaji wa majanga na tahadhari ya mapema umefanikiwa kutokana na mradi ulioanzishwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupunguza Madhara ya Maafa katika Kanda ya Afrika na kufadhiliwa na Serikali ya Nchi ya Italia kupitia Shirika la Maendeleo la Italia (Italian Agency for Development Cooperation) ambapo Taasisi ya CIMA Research Foundation ya Italia imesadia kutoa utaalam wa utekelezaji wa shughuli zote.

Kufuatia umuhimu wa kituo hicho, Dkt. Yonazi ametoa wito kwa nchi  wanachama pamoja na  mataifa mengine kuja Tanzania kwa lengo la  kujifunza na kubadilishana uzoefu kwa kuzingatia umuhimu wake.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoshiriki katika kikao hicho cha siku nne ambacho kimefanikiwa kuwakutanisha wadau zaidi ya elfu moja wa  maafa kwa nchi za Afrika  wakiwemo wataalamu kutoka  katika ngazi za kitaifa, Serikali za mitaa, Mashirika ya Umoja wa Kitaifa na Kimataifa, Asasi za Kiraia, sekta binafsi, taasisi za elimu na utafiti na waandishi wa habari.



Chapisha Maoni

0 Maoni