Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Dkt. Eblate Mjingo amepongeza mradi wa utafiti wa Uandaaji Ramani za kubainisha makimbilio ya wanyamapori (Refugia) kwa miaka ijayo kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia ya nchi uliofanywa na watafiti kutoka chuo cha Massachusetts- Marekani kwa kushirikiana na watafiti wa TAWIRI.
“Ramani hii itasaidia mamlaka husika
kuhifadhi maeneo hayo yaliyobainishwa, hivyo kuhakikisha ustawi wa wanyamapori
wakati wote,” amefafanua Dkt. Mjingo.
Dkt. Mjingo ameoa wito kufanyika tafiti zaidi za
mabadiliko ya tabia ya nchi zilizojikita katika
uhifadhi wa wanyamapori kwani bado kuna ombwe “Mabadiliko ya tabia ya nchi hayawaathiri
binadamu pekee na mimea, hivyo kuna uhitaji mkubwa wa watafiti kuangazia mabadiliko ya tabia ya nchi kwa
wanyamapori ili kushauri nini kifanyike
kuhifadhi rasilimali hii.”
Aidha, Dkt. Mjingo amesema Tanzania
imeendelea kuwa makazi pendwa ya spishi mbalimbali za Wanyamapori kutokana na
uhifadhi mzuri sambamba na hali ya hewa.
“Kutokana na hali nzuri ya uhifadhi,
wanyamapori wahamao mfano nyumbu katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wamekuwa
wakibaki ndani ya maeneo yao kwa muda mrefu na pale wanapohama hurejea mapema
sana,” ameainisha Dkt. Mjingo.
Naye Dkt. Toni Lyn Morelli, mtafiti
kutoka Chuo cha Massachusetts - Marekani akiwasilisha matokeo ya utafiti ya mradi huo wa ''Climate
Adaptation for Biodiversity Conservation in the Face of Climate Change in
Tanzania, amesema kwa kuzingatia nchi ya Tanzania ni makazi ya bioanuwai kubwa,
utafiti huu ni kwanza kufanyika barani Afrika hivyo kuifanya Tanzania kuwa ya
kwanza kuwa na ramani inayoainisha maeneo ya makimbilio ya wanyamapori miaka
ijayo kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia ya nchi.
Wasilisho hili limefanyika katika
ukumbi wa makao makuu ya TAWIRI na kuhudhuriwa na watafiti wabobezi katika
njanja mbalimbali wa TAWIRI akiwemo Wakurugenzi wa Vituo vya Utafiti.
0 Maoni