TAWIRI yahimiza tafiti za mabadiliko ya tabia ya nchi kwa wanyamapori

 

Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Dkt. Eblate Mjingo amepongeza mradi wa  utafiti  wa  Uandaaji Ramani za kubainisha makimbilio ya wanyamapori (Refugia) kwa miaka ijayo kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia ya nchi uliofanywa na watafiti  kutoka chuo cha Massachusetts- Marekani kwa kushirikiana na watafiti wa TAWIRI.

“Ramani hii itasaidia mamlaka husika kuhifadhi maeneo hayo yaliyobainishwa, hivyo kuhakikisha ustawi wa wanyamapori wakati wote,” amefafanua Dkt. Mjingo.

Dkt. Mjingo  ameoa wito kufanyika tafiti zaidi za mabadiliko ya tabia ya nchi zilizojikita katika  uhifadhi wa wanyamapori kwani bado kuna ombwe  “Mabadiliko ya tabia ya nchi hayawaathiri binadamu pekee na mimea, hivyo kuna uhitaji mkubwa wa watafiti  kuangazia mabadiliko ya tabia ya nchi kwa wanyamapori ili kushauri nini kifanyike  kuhifadhi rasilimali hii.”

Aidha, Dkt. Mjingo amesema Tanzania imeendelea kuwa makazi pendwa ya spishi mbalimbali za Wanyamapori kutokana na uhifadhi mzuri  sambamba na hali ya hewa.

“Kutokana na hali nzuri ya uhifadhi, wanyamapori wahamao mfano nyumbu katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wamekuwa wakibaki ndani ya maeneo yao kwa muda mrefu na pale wanapohama hurejea mapema sana,” ameainisha Dkt. Mjingo.

Naye Dkt. Toni Lyn Morelli, mtafiti kutoka Chuo cha Massachusetts - Marekani akiwasilisha  matokeo ya utafiti ya mradi huo wa ''Climate Adaptation for Biodiversity Conservation in the Face of Climate Change in Tanzania, amesema kwa kuzingatia nchi ya Tanzania ni makazi ya bioanuwai kubwa, utafiti huu ni kwanza kufanyika barani Afrika hivyo kuifanya Tanzania kuwa ya kwanza kuwa na ramani inayoainisha maeneo ya makimbilio ya wanyamapori miaka ijayo kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia ya nchi.

Wasilisho hili limefanyika katika ukumbi wa makao makuu ya TAWIRI na kuhudhuriwa na watafiti wabobezi katika njanja mbalimbali wa TAWIRI akiwemo Wakurugenzi wa Vituo vya Utafiti.



Chapisha Maoni

0 Maoni