Muhimbili Mloganzila yapokea msaada kutoka Korea

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila imepokea vifaa tiba mbalimbali kutoka Africa Future Foundation kwa kushirikiana na Jeju National University Hospital, msaada ambao utasaidia kuendelea kuimarisha na kuboresha huduma za matibabu kwa wagonjwa wanaofika hospitalini hapa.

Vifaa tiba hivyo vitatumika kuendelea kuboresha huduma za dharura kwa wagonjwa, wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji, kufuatilia mienendo ya wagonjwa baada ya kufanyiwa upasuaji ili kuhakikisha afya zao zinaendelea kuimarika kwa wakati.

Akipokea msaada huo, Naibu Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Julieth Magandi ameshukuru kwa msaada huo kwani umekuja wakati muafaka na pia utaongeza ufanisi katika kutoa huduma na kuwafanya wananchi kuendelea kupata huduma bora.

Dkt. Magandi ameongeza kuwa Taasisi kutoka Korea Kusini zimekuwa na ushirikiano wa manufaa makubwa na Muhimbili Mloganzila kwa kusaidia katika maeneo ya kuwajengea uwezo wataalam, kuleta wataalam kutoka Korea kwa lengo la kubadilishana uwezo pamoja na kutoa msaada wa vifaa tiba.

Kwa upande wake Meneja Mradi wa Africa Future Foundation Seong Hong amesema taasisi yake kwa kushirikina na Jeju National University Hospital wataendelea kutoa misaada kwa hospitali hii ili kuhakikisha Watanzania watapata huduma bora za afya.

Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila imekuwa na ushirikiano wa muda mredu na taasisi za Korea Kusini ikiwemo Korea Foundation for International Health Care (KOFIH), Africa Future Foundation (AFF), Vision Care na Jeju National University Hospital.

Chapisha Maoni

0 Maoni